Wednesday, September 24, 2014










BINADAMU ni kiumbe ambaye ameumbwa na tabia nyingi. Miongoni mwa tabia hizo ni kutoridhika na hali aliyokuwa nayo, au kile anachopata.

Siku zote binadamu akiwa mnene atatamani apungue na kuwa mwembamba, mwembemba atamani unene. Maskini atatamani kuwa tajiri. Lakini, hali ni tofauti kwa binadamu anayeitwa Peng Shuilin, mkazi wa kitongoji cha Hunan, China.

Shuilin mwenye umri wa miaka 39, amepoteza sehemu kubwa ya mwili wake; amebaki na mikono, tumbo na kichwa tu, lakini anaishi maisha ya raha na kukubali kila ambacho Mungu amemjaalia.

Shuilin alipoteza viungo vyake katika ajali mbaya ya gari iliyotokea mwaka 1995, akiwa kwenye kitongoji cha Shenzhen, ambapo tairi za gari hilo kubwa lililokuwa na mizigo lilipita kwa bahati mbaya kiunoni mwake na kufyeka viungo vyote na kubaki nusu. Ndio maana mwenyewe anajiita 'binadamu nusu.'

Baada ya ajali hiyo mbaya hakuna aliyeamini kama Shuilin angeweza kuendelea kuwa hai, na alilazimika kukaa hospitali iliyopo Shenzhen, Kusini mwa China, kwa miaka miwili ili kupatiwa matibabu ya karibu zaidi kutokana na upasuaji mkubwa aliofanyiwa kurekebisha mawasiliano ya mwili wake na viungo vilivyosalia.

Hivi sasa Shuilin kwa kutumia sehemu ya mwili wake uliobaki, anaweza kufanya mazoezi, anaweza kutumia mikono yake anayoitegemea kwa shughuli zake ndogo ndogo kuanzia mwanzo wa siku hadi anapoingia kitandani kujipumzisha.

Ni miaka 19 sasa imepita tangu alipopata ajali hiyo mbaya, Shuilin ameongezewa viungo vingine bandia vya mwili wake ambavyo anaendelea kuvifanyia mazoezi akiwa na madaktari wake.

“Tumemfanyia uchunguzi, yupo imara kama ilivyo kwa wanaume wa umri wake" anasema mmoja wa madaktari wanaomtibu Shuilin.

Kutokana na nafuu aliyopata, Shuilin amefungua duka lake kubwa la kuuza bidhaa mbalimbali ambalo lina utaratibu tofauti na mengine; dukani kwake kila kitu kinauzwa kwa nusu ya bei ya kawaida na anaruhusu mapatano ya bei. Duka hilo amelipa jina la "binadamu nusu, bei nusu."

Shuilin mwenye sentimita 78, amekuwa maarufu nchini mwake na hata nje ya China, amekuwa mfano wa kuigwa kwa watu wengi. Kwa kutumia baiskeli yake maalumu inayotumiwa na watu wenye ulemavu 'wheel chair' anaweza kuhudumia wateja wake bila wasi wasi na muda wote anaonekana mwenye furaha na asiyejali matatizo makubwa yaliyomkuta.

Watu wengi wanashangaa kumuona akiwa katika hali hiyo, jambo ambalo limewabadilisha mitazamo yao hasa kwa wale waliokuwa wamekata tamaa ya maisha huku wakiwa wamekamilika viungo.

Ni baada ya watu hao kujiuliza, kama mlemavu aliyekatika sehemu kubwa ya mwili wake anaishi maisha ya furaha na amefanikiwa kimaisha, kwanini wao wasio na kasoro washindwe? Simulizi ya Peng Shuilin inasikitisha, lakini inafundisha.

0 comments:

Post a Comment