Friday, October 17, 2014

unnamedMwakilishi wa FAO nchini Tanzania Diana Templeman kushoto akisakata Rumba  mziki uliokuwa ukiporomoshwa na Bendi ya Katavi Jazii na Mkuu wa Mkoa wa Katavi Dkt Rajabu Rutengwe siku ya Maazimisho ya Chakula Duniani Kitaifa yaliyofanyika Mkoani Katavi.

………………………………………………………………………….
Na Kibada Ernest-Katavi
 Serikali imesema ni aibu kubwa na jambo la fedheha kwa Taifa  kuendelea  kukabiliwa na janga la udumavu  linalotokana na  ukosefu  wa lishe bora  na matunzo sahihi.
Hayo yamesemwa na  Waziri wa  Kilimo, Chakula na  Ushirika  Mhandisi Christopher   Chiza  katika hotuba yake  iliyosomwa   siku ya  Chakula Dunian  kwa niaba yake na Mkuu wa Mkoa wa Katavi  Dkt. Rajab Rutengwe .
Amesema  ni jambo   lisilovumilika  kuendelea   kupoteza  maisha ya zaidi ya watoto 130  na mama  wajawazito  kila siku  kwa ukosefu wa lishe bora  na  ukuaji wa kiakili wa watoto , kupunguza uwezo  wa kufanya  vizuri   shuleni  na  kupunguza ufanisi  katika maisha  ya utu uzima.
Amewaasa  wadau  kushirikiana  na Serikali  katika   kuhamasisha uboreshaji  wa lishe  miongoni mwa  familia  na  taifa kwa ujumla,Akaongeza kuwa   kwa mujibu wa viwango vya ulaji  wa mazao ya mifugo  Nchini ni wastani wa kilo 12 za nyama , lita 45 za maziwa na mayai 75  za mayai kwa mwaka.
Amesema   bado viwango hivi vipo chini   ukilinganisha  na viwango  vinavyopendekezwa  na Shirika la Chakula na Kilimo  Duniani   ambavyo ni  wastani wa kilo 50 za nyama, lita 200 za maziwa  na mayai 300 kwa mwaka,lakini kwa Mkoa wa Katavi  hali ni mbaya.
Awali Mwakilishi wa Shirika la Chakula duniani   nchini  Tanzania Diana Tempelman  amesemakuwa wakulima wa kaya hasa wazalishaji wadogo wadogo ni sehemu ya asilimia 70 ya wakazi duniani wasio na chakula cha kutosha ambao wanaishi katika maeneo ya vijijini.
Akaongeza kuwa familia za wakulima zina nafasi kubwa  ya kupiga hatua iwapo zitawezeshwa kwa wakati na kutatua changamoto zinazowakabili.
Templeman alisema kuwa watu wanaokaribia milioni 75 ambao hawana chakula  cha kutosha hivyo jitihada zaidi zinahitajika,nchi 63 zinazoendelea tayari zimefikia malengo ya millennia katika kukabiliana nautapiamlo mkali ifikapo  2015.
    Kwa upande wake Naibu Katibu Mkuu wa Chakula Kilimo na Ushirika Mhandisi Raphael Daluti akitoa salamu za wizara ameeleza kuwa wakati ikiazimishwa siku ya chakula duniani nchi imezalisha chakula cha kutosha mahitaji na kupata ziada kubwa.
Tathimini za awali ya uzalishaji wa mazao ya chakula kwa msimu wa mwaka 2013/2014 na hali ya chakula kwa mwaka 2014/2015 inaonesha uzalishaji ni tani milioni 16.02 kati ya kiasi hicho tani milioni  9.8 ni za mazao ya nafaka na tani milioni 6.2 ni za mazao yasiyo nafaka. Kauli mbiu mwaka huu kilimo cha kaya lisha dunia Tunza Mazingira.

0 comments:

Post a Comment