Wednesday, October 15, 2014



ROMA, Italia
KATIKA hatua inayooonekana kuwa tofauti na matarajio ya wengi kutokana na msimamo wake, Kanisa Katoliki hivi sasa linaelekea kwenye hatua za mwisho za kuukubali ushoga.

Hii inatokana na mkutano wa wakuu wa Kanisa hilo duniani kutoa wito kwa waumini wake duniani kuwachukulia watu wanaofanya mapenzi ya jinsia moja kama watu walio na haki na sawa na wengine.

Kauli hii imechukuliwa na watu wengi na hasa wale wanaoshabikia ushoga duniani kusema kwamba kanisa hilo hivi sasa linaukubali ushoga.

Aidha, kauli hii inakuja baada ya Maaskofu kuandika ripoti wakati wa mkutano wa synodi ukiendelea huko Vatican na kusema kuwa wapenzi wa jinsia moja wana zawadi na viwango vya kutoa kwenye jumuiya za kikristo hii ikiwa ni ripoti iliyotolewa mapema wiki hii.

Msimamo huo mpya wa Kanisa Katoliki, unaonekana kuwakera watu wenye msimamo mkali kwenye kanisa hilo na moja ya makundi yenye kushikilia msimamo mkali ki-kanisa wametupilia mbali ripoti hiyo na kuiita ya kisaliti.

Zaidi ya maaskofu 200 wa Kanisa Katoliki wanakutana kwenye mkutano wa synodi tangu mapema mwezi huu, katika mkutano huo ni papa Francis aliyetoa mwito wa kujadili masuala ya utoaji wa mimba, vidonge vya uzazi wa mpango, mapenzi ya jinsia moja na talaka.

Papa Francis amewataka viongozi wa juu wa kanisa hilo kuzingatia zaidi suala la wapenzi wa jinsia moja katika mtazamo chanya kuliko kuwa kinzani na amefanikiwa kuwateka maaskofu wanaohudhuria mkutano huo wa sinodi.

Mwaka uliopita katika ripoti aliyoitoa papa Francis kuhusiana na mwenendo wa Kanisa Katoliki kuwa waumini walio wengi waliliacha mkono kanisa hilo kutokana na mafunzo yanayohusu ngono na dawa za uzazi wa mpango.

Papa huyo anazichukulia ndoa hizo za jinsia moja kama zisizo na utaratibu akiinukuu ripoti ya kanisa katoliki iliyochapishwa mwaka 1986, wakati Papa Francis alipokua mshauri mkuu wa masuala ya teolojia ya Kanisa Katoliki wa hayati papa John Paul wa pili.

Moja ya sababu zilizodaiwa kumuondoa kitini mtangulizi wa Papa Francis, Papa Benedict, ilielezwa kwamba ulikuwa ni mvutano kati yake na genge la wapenda ushoga ndani ya uongozi wa kanisa hilo huko Vatican.

Ilielezwa Benedict alikuwa ameshikilia msimamo wake kwamba kanisa hilo linapaswa kusimamia mafundisho halisi ya kanisa ya kupiga marufuku ushoga kama yalivyo kwenye Agano la Kale.

Nguvu kubwa ya vikundi vya kutetea haki za watu wenye mapenzi ya jinsia moja ni juu ya kauli ya papa Francis aliyoitoa mwishoni mwa mwaka wa jana alipokuwa kwenye kambi ya vijana wa kanisa hilo huko Rio de Jeneiro alitoa kauli kuwa kama mtu anamtafuta Mungu na ana nia njema, yeye ni nani wa kuhoji?

Msimamo huo mpya wa Kanisa Katoliki, huenda ukapata upinzani mkali kutoka kwa waumini wa kanisa hilo barani Afrika, ambako mapenzi hayo yamechukuliwa kiasili kama laana na matendo ambayo hata wanyama hawawezi kuyafanya.

Mara ya kwanza zilipojitokeza dalili za kuruhusiwa kwa mapenzi hayo na kanisa, viongozi wote wa kanisa hilo barani Afrika walieleza wazi upinzani wao.

Hata wakati Rais Barack Obama alipozungumzia haki za kuwaruhusu watu kufanya mapenzi ya kishoga, alipingwa na bara lote la Afrika likiwemo Kanisa Katoliki la nchini Kenya ambapo Kadinali John Njue alisema hilo ni jambo ambalo halitakubalika.

Hata hivyo, katika hali ya kutaanisha, kanisa hilo limesema halitafungisha ndoa za mashoga. Limesema kinachotakiwa ni kutowakana waumini wao wanaojishughulisha na ushoga kuwahusisha kundini.

Baadhi ya waumini wake wenye msimamo mkali wanaona kauli hiyo kama iliyo sawa nakuruhusu uzinzi katika kanisa hilo, ambalo hata wale walioolewa na watu wasio waumini wa kanisa hilo wamekuwa wakichukuliwa kama wazinifu kiasi cha kutoshiriki ulaji wa mkate wa bwana.

Taarifa zaidi za mkutano huo zinasema, Maaskofu hao hawajesema kuwa wanaounga mkono ndoa za jinsia moja, lakini Mashirika yanayotetea haki za mashoga na wasagaji wanasema hatua ya kutambuliwa na Kanisa Katoliki ni ya kutia moyo.

0 comments:

Post a Comment