Thursday, September 17, 2015

Lowassa: Nipeni bakora niwatandike mafisadi.
Mgombea wa urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa tiketi ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Edward Lowassa

Mgombea wa urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa tiketi ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Edward Lowassa, amefunguka na kuwaomba Watanzania kumpa kura ambazo ameziita bakora ili awacharaze viboko watu wote wanaojihusisha na vitendo vya ufisadi nchini.

Lowassa ambaye anaungwa mkono na vyama vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), alitoa kauli hiyo jana alipokuwa akihutubia umati katika mkutano wa kampeni kwenye Shule ya Msingi Kiwanja cha Ndege, mjini Morogoro.
Alisema ili kutekeleza azima yake, ni vizuri wananchi wakajitokeza kwa wingi kama Oktoba 25, mwaka huu kama walivyojitokeza jana wapige kura ili kumpa kazi ya kuwanyoosha mafisadi.
Akizungumza huku akikatizwa kutokana na kushangiliwa na umati, Lowassa alisema Serikali yake itahakikisha inawashughulikia wale wote watakaotumia vibaya fedha au madaraka waliopewa kinyume cha sheria na taratibu.
Lowassa alijiuzulu nafasi ya uwaziri mkuu mwaka 2008, kama njia ya kuwajibika baada ya kuibuka kwa sakata ya serikali kuipa zabuni kampuni ya kufua umeme ya Richmond katika mazingira tata.
Sakata hilo liliibuliwa na Kamati Teule iliyoongozwa na Mbunge wa kyela, Dk. Harrison Mwakyembe, baada ya kuchunguza na kuwasilisha ripoti bungeni
Source: Nipashe



0 comments:

Post a Comment