Monday, October 5, 2015

 Tunawakaribisha sana ndugu na wadau wetu waandishi wa habari toka vyombo mbali mbali  kwa kuja na kushiriki nasi katika mkutano wetu huu nuhimu Makao Makuu ya UVCCM leo oktoba 5 2015.
Tumewaita kwa sababu kadhaa muhimu za kisiasa tukiamini na kutegemea mtafikisha ujumbe wetu kwa jamii kama mnavyotimiza  wajibu  wa kazi zenu ngumu na nzito za kitaaluma za kila siku.
Hata hivyo UVCCM  tunawashukuru kwa dhati  waandishi wa habari nyote kwa kazi kubwa mnazozifanya za kuihabarisha jamii kuhusu mwenendo bora  wenye mafanikio  kwa maendeleo ya kampeni zinazofanywa na mgombea wetu wa urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa tiketi ya CCM  Dk. John Pombe
Magufuli na Mgombea Mwenza wake Ndg. Samia Suluhu Hassan.
Vile vile tunawapongeza kwa namna ya pekee  jinsi mnavyotuhabarisha na kutupasha kuhusu maendeleo ya kampeni za mgombea wetu wa urais wa  Zanzibar Dk Ali Mohamed Shein sambamba na  wagombea  wetu wa ubunge, uwakilishi na madiwani Tanzania Bara na Zanzibar.
Ndugu waandishi wa habari


Kwa namna  moja maendeleo ya kampeni za chama chetu zinakwenda vizuri hasa upande wa Tanzania Bara lakini huko Zanzibar kidogo kumejichomoza vitendo vya kihuni vinavyofanywa na wafuasi wa vyama upinzani.


Kati ya tarehe 15  na 18 Septemba  Mwaka huu misafara ya wanachama wa CCM  katika maeneo ya  Kuyuni, Mtuhaliwa na Chokocho katika  Mkoa wa Kusini Pemba, imeshambuliwa kwa kupigwa mawe wakati wakirejea toka kuhudhuria  mikutano ya kampeni, baadhi ya watu wamejeruhiwa na kupata majeraha ikiwemo  gari moja kuvunjwa kioo cha mbele.

Kitendo hicho ni cha  kihuni, UVCCM tunakilaani kwa nguvu zetu zote  lakini pia hayo ni matokeo ya hotuba za Katibu Mkuu wa CUF   Seif Sharif Hamad ambaye mara kadhaa amekuwa akisema mwaka huu vijana wake hatawaonya watakapotaka kufanya jambo lolote, hatawazuia wala kuwaasa.

UVCCM tunamkanya Seif na CUF kuacha  mara moja tabia ya kutaka  kumshika paka sharubu, paka mara zote huchezewa maeneo mengine ya mwili wake si sharuhu zake, ukimshika  sharuhu atakuparamia usoni, kukuparua na pengine hata  kudhuru macho yako.

Kufikiwa kwa Maridhiano ya Kisiasa kati ya CCM na CUF huko Zanzibar  lengo lilikuwa kuendesha siasa za kiungwana, kistaarabu na kuvumiliana. Kuondosha  siasa za mti kwa macho, hasama na  kuzika chuki.


Ikiwa CUF  wameleweshwa na ustawi wa amani iliopo sasa Zanzibar tokea kuundwa Serikali ya Umoja wa Kitaifa, hatutaona muhali, shida wala kikwazo cha  kurejea tena katika zama ya  vuta nikuvute ile ile iliokuwepo kabla ya kufikiwa maridhiano ya kisiasa.


Ndugu Waandishi wa habari.


Jambo jingine ni kuhusiana na Mzee  Kingunge Ngombale Mwiru jana Septemba 4 mwaka huu  kutangaza kuihama CCM huku  akitoa matamshi ya kukisakama na kukiponda chama chetu  akiwa hana nguvu ya hoja.
Itakumbukwa Agosti 15 mwaka huu Baraza kuu la Taifa la UVCCM lilimvua wadhifa wa Ukamanda Mkuu wa Jumuia yetu baada ya kutoridhishwa na mienendo ya mwanasiasa huyo baada ya jumuiya  yetu kumpima na kumlinganisha na mwanasiasa mwenye akili zinazofanana na mbayuwayu.

UVCCM  wakati tukitoa  uamuzi wetu,   wapo  baadhi ya watu wakiwemo  wanasiasa walibeza na kuona kama tulimuonea au kumdhalilisha Mzee Ngombale.
Nataka nieleze bayana kuwa  kabla ya kumvua ukamanda wa UVCCM  tulimtathmini,  tulimchambua na kumkuta tayari amepotea njia na kumkuta kwa hiari yake  akiamua kujivika joho la utumwa na kujitolea kumtumikia shetani ili kujaza tumbo lake na si uaminifu tena kama alivyokuwa akiheshimika hapo awali tokea enzi za TANU na ASP kabla ya kuzaliwa Chama Cha Mapinduzi mwaka 1977.
Mwanasiasa huyo ametoa porojo huku akipapatua kwa lengo la kutaka kuionyesha hadhira kuwa CCM si chama makini akisahau katika uhai na maisha yake yote amekuwa akisema hakitatokea chama bora nchini, kuishinda na kitakacholingana na CCM.
Tokea akiwa kijana mdogo kabisa Mzee Kingunge amekuwa mwanachama wa jumuiya yetu hadi kufikia kuwa  Katibu Mkuu wa  Pafmeca Youth iliokuwa na Makao makuu yake nchini Algeria
Kilichotokea ni kwamba Mzee  Kingunge ameshindwa kuheshimu matokeo ya mchuano wa nguvu ya hoja ndani ya chama chetu huku akitaka kulazimisha fikra zake ndizo zionekane sahihi na za wenzake zikikosa maana na umuhimu wowote.

 Kimsingi huo si uungwana katika dhana  ya siasa, huo  ni uimla na ufashisti usiokubalika katika siasa za kileo. Alifikiri CCM ni mtu, umbo na uso wake, si taasisi pia akidhani mtu mwenyewe ni yeye na si wengine  au maamuzi yatokanayo na vikao vya kikatiba akiviona havina maana wala uzito kuliko fikra na utashi wake binafsi.

Anaposema  taratibu za kumpata mgombea zilikiukwa sijui ana maana ipi wakati yeye hakuwa mjumbe wa NEC, Kamati Kuu ya CCM na wala  Mkutano Mkuu wa Taifa.
Chama chetu hakiwezi kuendeshwa kinyume na taratibu za Katiba ya CCM kama anavyodai na kufikiri Mzee Kingunge hasa katika mchakato wa kumpata mgombea wa chama chetu kwa nafasi ya urais.

Mzee Kingunge toka awali amekataa kujiegemeza  katika kuamini na kusimamia taratibu za kumsaka na kumpata mgombea wetu wa urais kulingana na sifa za msingi badala yake akimtaka mtu hata kama mgombea huyo ameopungukiwa sifa na vigezo vya kuwa mgombea bora wa urais na  mwenye sifa zinazolingana na hadhi ya chama chetu.
Lilipokatwa jina la Edward Lowassa Mzee Kingunge akawa mbogo, asiejenga nguvu ya hoja ila akiandaa mipango na  mazingira ya kukitishia nyau chama chetu ili kimuogope na kuyaridhia matakwa yake.

Mzee Kingunge ameshindwa kuelewa na kukubali  ukweli kama urais ni taasisi adhim yenye staha na hakutaka aamini kama   urais si kama mchezo wa   bao au karata ila ni vigezo, sifa njema na amana kwa  mgombe mhusika katika jamii inayomtazama na kumtegemea

Anaposema taratibu CCM  zimekiukwa, hazikuwa sahihi na kinyume na demokrasia, tunamuuliza hivi kilichofanyika chadema hadi kumpa mgombea wa urais ndiyo mchakato makini wa demokrasia anayoitamani?
UVCCM tunaungana na kukubaliana na uamuzi wa vikao vya chama chetu uliofuatwa kwa mujibu wa kanuni, taratibu na katiba yetu katika  kumpata na kumteua mgombea wa urais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na mgombea urais wa Zanzibar.
Chama chetu kitabaki kuwa ni  imara daima, kitahimili na kukabiliana na misukosuko na dhoruba za kisiasa na kwamba  wakati wote tunaamini hakuna mwanachama au kiongozi mmoja ambaye ni  muhimu au  bora kuliko mwingine

Mzee Kingunge amewahi kutoka dini na kusema hakuna mungu  haikuwa lolote, sasa amehama CCM si jambo la ajabu, hata akiamua kusaliti na kujitoa kwenye kabila lake bado atahesabika ni Mtanzania wala hayupo mtu atakaemshtua au kumshangaa.

Ahsanteni kwa kunisikiliza.




"KIDUMU CHAMA CHA MAPINDUZI "


SHAKA HAMDU SHAKA (MNEC)
KAIMU KATIBU MKUU UVCCM

0 comments:

Post a Comment