Fundi Kevin Omollo akiwa mbele ya CT-SCAN inayodaiwa kuwa katika matengenezo huku akitoa maelekezo kwa Balozi Sefue sambamba na baadhi ya viongozi kutoka Wizara ya Afya.
KATIBU Mkuu Kiongozi, Balozi Ombeni Sefue leo ametembelea katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili na kukagua Mashine za MRI CT-Scan ikiwa ni ziara ya mrejesho wa pili wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk. John Pombe Magufuli wakati alipotembelea hospitalini hapo na kukuta mashine hizo zikiwa mbovu.
Balozi Sefue amezikuta mashine hizo zikiwa bado kwenye matengenezo ambapo mafundi kutoka nchini Kenya ambao ndiyo wasambazaji wa bidhaa za Philips walikuwa wakitengeneza, hivyo wakaahidi kuwa baada ya siku mbili mashine ya MRI itakuwa imetengemaa na CT-Scan kufikia siku ya Alhamisi itakuwa nayo imetengemaa.
Balozi Sefue mara baada ya kupata maelekezo hayo amewatahadharisha kutoendelea kupata tena usumbufu wa mashine hizo na kusema hatua kali zitachukuliwa endapo watafanya mzaha dhidi ya mashine hizo.
Baada ya ukaguzi wa mashine hizo, Balozi Sefue alitembelea kwenye jengo jipya la kitengo cha Taasisi ya Tiba ya Mifupa na Mishipa ya Fahamu (Moi) kuangalia vitanda vilivyonunuliwa kutokana na agizo la Rais Magufuli kuamuru pesa zilizokuwa zimeandaliwa kwa ajili ya bajeti ya sherehe za ufunguzi wa Bunge 11 la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dodoma alhamisi iliyopita kupelekwa kununulia vitanda Muhimbili.
(STORI: DENIS MTIMA NA MAYASA MARIWATA/GPL
0 comments:
Post a Comment