Friday, December 18, 2015




Siku moja baada ya kuahirishwa ziara ya aliyekuwa mgombea urais kupitia Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Edward Lowassa, chama hicho kimesema hakilitambui zuio la kufanya maandamano na mikutano ya kisiasa lililowahi kutolewa na Mkuu wa Jeshi la Polisi, Inspekta Jenerali (IGP) Ernest Mangu mwezi uliopita.

Kauli ya Chadema ilitolewa jana na Ofisa Habari wa chama hicho, Tumaini Makene, baada ya kuulizwa juu ya kuwapo taarifa kuwa wameshindwa kuendelea na ziara ya Lowassa kutokana na zuio hilo.

Akizungumza Dar es Salaam jana, baada ya kuahirishwa mkutano na waandishi wa habari, Makene alisema katazo hilo la mikutano ya hadhara linaendelea.

“Hatulitambui tamko la IGP, sisi tuliahirisha kutokana na kutingwa na shughuli za uchaguzi mdogo, hivyo tukimaliza kushughulikia masuala hayo ya uchaguzi, tutarudi kuendelea na ziara kama tulivyopanga nchi nzima. Hata kama IGP kakataza, mbona CCM wanafanya mikutano ya hadhara?” alisema Makene.

Akizungumzia sababu za kuahirisha mkutano ambao chama hicho kiliuitisha jana na kusababisha waandishi wa habari kusubiri kwa zaidi ya saa tatu, Makene alisema kuna masuala ya msingi ambayo yalijitokeza katika suala la umeya wa Jiji la Dar Salaam ambalo ndilo lilikuwa ajenda.

0 comments:

Post a Comment