Wednesday, December 23, 2015

SERIKALI imesisitiza azma yake ya kufanya mabadiliko ya watendaji wa Wizara ya Nishati na Madini na TANESCO kufuatia kushamiri kwa urasimu na kukosa ubunifu.



Imesema hatua hiyo imetokana na baadhi yao kukosa ubunifu katika uanzishaji na uendelezaji wa miradi ya umeme na kusababisha majadiliano ya mikataba ya uzalishaji umeme kuchukua muda mrefu.

Aidha, ilisema kwa vyovyote gharama za umeme lazima zipungue, hivyo imeziagiza Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA) na TANESCO kuwasilisha mapendekezo kupitia upya gharama hizo.
Akizungumza Dar es Salaam, jana, Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo, alitoa wito kwa watu na taasisi binafsi nchini kwenye uzalishaji umeme ili kuhakikisha nchi inakuwa na umeme wa uhakika na wa gharama nafuu.

Profesa Muhongo aliyasema hayo wakati wajumbe wanaounda Shirikisho la Viwanda Tanzania (CTI), Taasisi ya Sekta Binafsi Tanzania (TPSF) na Chama cha Wafanyabiashara, Wenye Viwanda na Wakulima (TCCIA) walipofi ka kuwasilisha changamoto mbalimbali za umeme wanazozipata katika utekelezaji wa majukumu yao.

Alisema serikali inakaribisha wawekezaji wazalishe umeme kwenye miradi midogo ya maji isiyozidi megawati 10 ambayo itasadia wananchi walio nje ya gridi ya taifa kupata umeme.

Aliitaja miradi mingine ambayo wawekezaji wana fursa ya kuwekeza kuwa ni uzalishaji umeme kwa kutumia nguvu ya upepo, jua, jotoardhi, mawimbi, tungamotaka, na bayogesi.

Alielezea lengo la serikali la kutaka kuzalisha umeme kwa kutumia makaa ya mawe ambapo kuna tani zaidi ya bilioni 9 ambako alizialika tasisi hizo binafsi kushirikiana na serikali kwenye uzalishaji huo.

0 comments:

Post a Comment