Friday, January 15, 2016




MFANYABIASHARA Morris John ‘Maliyanga’ (46) na wenzake watatu, wamepandishwa kizimbani katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, kujibu shitaka la unyang’anyi wa kutumia silaha wa vitu mbalimbali zikiwemo dola za Marekani zenye thamani ya sh. milioni 18.5.

Maliyanga, mkazi wa Mbezi Beach, Dar es Salaam, dereva pikipiki Frano Msaru au Singu (23) na wafanyabiashara Jeremiah Flavian (26) wakazi wa Sinza na Sandru Kamugisha (39), mkazi wa Kijitonyama, walifi kishwa mahakamani hapo jana.

Washitakiwa hao walipandishwa kizimbani mbele ya Hakimu Mkazi, Hellen Riwa, ambapo Wakili wa Serikali, Honolina Mushi, aliwasomea shitaka hilo. Akiwasomea shitaka hilo, Honolina alidai washitakiwa walitenda kosa hilo, Desemba 22, mwaka jana, maeneo ya Mabibo Ruhanga, wilayani Kinondoni, Dar es Salaam.

Alidai siku hiyo washitakiwa hao waliiba dola za Marekani 8,600 (sawa na sh. milioni 18.5), fedha taslim sh. milioni 2.5, kompyuta mpakato, simu nne za mkononi mali ya Anderson Aloyce.

Inadaiwa kabla na baada ya kutenda kosa hilo, washitakiwa hao waliwatishia Zeno Genes, Aneth Paulo na John Renatus kwa bastola ili waweze kufanikisha kupata vitu hivyo. Washitakiwa hao walikana shitaka hilo, ambapo Wakili Honolina, alidai upelelezi haujakamilika na kuomba shauri hilo kuahirishwa hadi tarehe nyingine kwa kutajwa.

Kwa upande wa mshitakiwa Msaru aliomba apewe kibali cha kwenda kutibiwa mguu kutokana na majeraha aliyodai kuyapata baada ya kupigwa akiwa polisi.

Hakimu alimtaarifu mshitakiwa huyo kwamba atapata matibabu kwa kuwa Jeshi la Magereza lina utaratibu wa kutoa huduma hiyo. Pia, aliahirisha shauri hilo hadi Januari 27, mwaka huu kwa kutajwa na kusema washitakiwa watarudishwa rumande kutokana na shitaka linalowakabili kutokuwa na dhamana kwa mujibu wa sheria.

0 comments:

Post a Comment