Sunday, January 10, 2016

 
 
 
Zaidi ya wakazi laki tatu kutoka kata zote 36 zilizoko halmashauri wilaya ya Chamwino mkoani Dodoma wanakabiliwa na baa la njaa kutokana na ukame wa muda mrefu ambapo hivi sasa wanalazimika kula wadudu jamii ya viwavi matunda ya porini, mizizi na uji wa ubuyu ili kujinusuru na vifo huku pia kukiwa na taarifa za watu watatu kupoteza maisha mmoja kati yao akijinyonga kwa sababu ya njaa.

Ni katika eneo la kata ya chamwino ikulu jirani na ikulu ndogo ya rais iliyopo wilayani hapa ambapo mama huyu na wakazi wengine kutoka maeneo mbalimbali wanalazimika kuja kushinda sehemu hii ili kujipatia angalau mlo ambao ni matunda aina ya zambarau , baadhi yao ambao wanadai tatizo la njaa ni kubwa wilayani humo hali inayochangia shughuli zingine ikiwemo za kilimo kusimama huku pia baadhi ya wazazi wakizikimbia familia.
 
Kufuatia tatizo hilo inawalazimu wajumbe wa baraza la madiwani wa jimbo la Chilonwa wilayani Chamwino kukutana ambapo viongozi hao wanashusha lawama kwa maofisa wa idara ya maafa chini ya ofisi ya waziri mkuu kuwa wameshindwa kuwasaidia wananchi licha ya kupokea taarifa mara kwa mara huku wakiishia kufanya tathmini na kutoa tani 150 tu za mahindi ambayo hata hiyo hayakidhi mahitaji.
 
Katika kuonyesha uhalisia wa tatizo la njaa Mussa Omari diwani wa kata ya majereko anaingia katika kikao hicho na mkebe wenye wadudu jamii ya viwavi jeshi ambao anadai yeye na wananchi wake walilazimika kuamka saa tisa usiku na kwenda porini kuwatafuta kwa ajli ya mlo.
 
Kwa upande wake afisa kilimo wa wilaya ya Chamwino Geofrey Nyamale anakiri kuwa baa la njaa ni kubwa wilayani humo kwani hali hiyo ilianza kujitokeza tangu mwezi may mwaka jana ambapo ofisi yake imekuwa ikifanya jitihada kubwa za kuomba chakula cha msaada lakini hawapati majibu sahihi kutoka ngazi za juu huku akibainisha kuwa msaada wa chakula unaohitajika hizi sasa ni zaidi ya tani 14000.
 

0 comments:

Post a Comment