HALMASHAURI ya Wilaya ya Tarime mkoani Mara imekataa kupokea hundi ya
takribani Sh bilioni 1.060 za malipo ya tozo ya huduma zilizotolewa na
kampuni ya Acacia ya uchimbaji wa madini katika Mgodi wa North Mara
wilayani hapa.
Mwenyekiti wa Halmashauri hiyo, Moses Yomami akitangaza uamuzi huo
katika ukumbi wa mikutano wa halmashauri, alisema wamegoma kupokea
malipo hayo kutokana na kukosekana taarifa sahihi ya kiasi halisi cha
dhahabu inayozalishwa katika mgodi huo.
Awali kabla ya Meneja wa mgodi huo, Garry Chapman kukabidhi hundi
hiyo, mwenyekiti huyo alimkatiza akisema kumekuwepo mapungufu makubwa
katika uwasilishaji wa fedha katika halmashauri hiyo ikiwa ni pamoja na
mrabaha na tozo ya ushuru katika siku za nyuma na kuzusha maswali kutoka
kwa madiwani juu ya uwazi wa kiasi halisi cha dhahabu kinachopatikana
baada ya uchimbaji.
Pia mwenyekiti huyo alieleza changamoto inayokabili halmashauri ya
kupata hasara wakati wa kuhamisha fedha hizo kuelekea katika akaunti ya
umma kutokana na malipo hayo kufanywa kwa dola za Kimarekani na kupata
hasara isiyo ya lazima kutokana na viwango vya ubadilishanaji kubadilika
kila mara.
Pia katika hatua nyingine alitaka kampuni hiyo iwasilishe orodha ya
kampuni tanzu zinazohudumu katika mgodi huo ili waweze kufanya tathmini
juu ya mchakato wa kampuni hizo pia kulipa ushuru wa huduma kama sheria
inavyoagiza ili kuongeza kipato cha halmashauri.

0 comments:
Post a Comment