Sunday, January 10, 2016




SERIKALI imetangaza utaratibu mpya wa utekelezaji wa mpango wake wa kubomoa nyumba zote zilizojengwa kinyume cha taratibu na sheria za nchi.

Imesema hivi sasa itajielekeza kubomoa nyumba zilizo ndani kabisa ya bonde, kwenye miteremko ya kuingia bondeni na katika kingo za Bonde la Msimbazi.

Sambamba na hilo, imesema itaheshimu uamuzi wa mahakama dhidi ya mashauri ya watu walioweka pingamizi la nyumba zao kubomolewa na itawalipa fidia wale wote waliojenga kwenye maeneo hatarishi kwa kupewa vibali halali na Serikali na pia itafuatilia kesi zilizoko mahakamani ili ziishe haraka tayari kwa taratibu nyingine kuendelea.

Uamuzi huo wa Serikali umetangazwa jana na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais, January Makamba, mbele ya waandishi wa habari wakati akitoa taarifa ya mkutano wa mawaziri watatu walioketi kufanya tathmini ya mwenendo wa kazi hiyo na kuibuka na maazimio 12 yanayoelekeza namna mpya wa utekelezaji wa ubomoaji.

Mawaziri waliofikia pamoja na Makamba kufanya tathmini hiyo ni Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, William Lukuvi, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais- Tamisemi, George Simbachawene na Naibu Waziri wa  Maliasili na Utalii, Injinia Ramol Makani.

Aidha, tangazo la uamuzi huo mpya wa Serikali limekuja ikiwa ni siku chache baada ya Rais John Magufuli kukutana kwa nyakati tofauti na marais wawili wastaafu, Benjamin Mkapa na Jakaya Kikwete pamoja na Waziri Mkuu mstaafu, Jaji Joseph Warioba.

Akizungumza na waandishi wa habari, Waziri Makamba alisema kazi ya kuwaondoa wananchi wanaoishi katika Bonde la Msimbazi itaendelea kwa utaratibu ambao hautawasababishia mateso na usumbufu.

Alisema utekelezaji wa kazi ya ubomoaji ndani ya bonde hilo utalenga makazi yote yaliyojengwa ndani kabisa ya bonde, kwenye miteremko ya kuingia bondeni na katika kingo za bonde.

Waziri Makamba alisema watu wenye nyaraka halali zilizowaruhusu kujenga walizopewa na mamlaka za umma hawatahamishwa bila kupewa sehemu nyingine za kujenga na kwamba watumishi wa umma waliotoa maeneo hayo watachukuliwa hatua za kinidhamu na kisheria.

Akizungumzia maeneo yaliyokwishabomolewa alisema katika muda wa siku tatu kuanzia jana, kazi ya kuzoa vifusi na kusafisha maeneo yaliyobomolewa itaanza.

Akizungumzia ukiukwaji wa taratibu dhidi ya baadhi ya maofisa wa Serikali, Waziri Makamba alisema Serikali itawachukulia hatua za kinidhamu watumishi wake wanaoendesha kazi ya kubomoa na kuweka alama ya X katika nyumba zinazopaswa kubomolewa kinyume na misingi ya sheria zinazotekelezwa.

“Serikali itawachukulia hatua za kinidhamu watumishi wake ambao watakwenda kinyume na misingi ya haki na uwazi, ikiwamo wanaoweka alama za X zaidi ya mita zilizowekwa kisheria, limeanzishwa dawati la malalamiko katika Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa ajili ya kupokea malalamiko au maswali kuhusu kazi hii.

“Pia nyumba na majengo yaliyokuwepo miaka mingi kabla ya kutungwa kwa sheria zinazotekelezwa sasa hayatabomolewa isipokuwa tu pale maisha ya watu yalipo hatarini,” alisema Makamba.

0 comments:

Post a Comment