Thursday, January 7, 2016


SERIKALI iko katika mazungumzo na viwanda vyote vinavyozalisha sukari kuangalia namna ya kuviondolea baadhi ya gharama za uzalishaji ili bidhaa hiyo ishuke bei.
 


Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji, Charles Mwijage alisema hayo jana alipofanya ziara katika Kiwanda cha Sukari cha Kagera na kuzungumza na uongozi pamoja na wafanyakazi wa kiwanda hicho.

Alisema wanalenga kuondoa gharama zisizo za lazima ili kupunguza bei ya sukari ambayo imeonekana kuwa kero kwa wananchi. Alisema Serikali ikiishakaa na wadau na itatoa jibu la kuridhisha kwa wananchi kwa maana ya kuwapa bei itakayowaridhisha na kwenda na hali halisi ya uchumi wa sasa.

Aidha Waziri Mwijage alisema ameridhishwa na uzalishaji unaofanywa na kiwanda hicho na akasema ni mfano wa kuigwa. Meneja wa Kiwanda hicho, Ashwin Lana alisema kimeajiri wafanyakazi 600 huku zaidi ya 400 wakiwa wa kudumu.

Wakati huo huo, wazalishaji, watumiaji wa sukari ya viwandani na ile ya matumizi ya nyum bani pamoja na wadau wote wa sukari nchini, wamepewa siku sita kupeleka taarifa za kiasi za sukari walichonacho kwenye hifadhi zao, ili kuhakikiwa kabla ya msimu wa kufunga viwanda haujaanza.

Kwa mujibu wa tangazo lililotolewa jana kwa vyombo vya habari na Bodi ya Sukari nchini (SBT), wahusika hao wanapaswa kuwasilisha taarifa zao kabla ya Januari 11, mwaka huu.

0 comments:

Post a Comment