Monday, January 25, 2016




BIDHAA mbalimbali zilizoingizwa nchini kutoka Marekani kwa ajili ya kutolewa msaada kwa Halmashauri ya Wilaya ya Tarime zimeteketezwa na Shirika la Viwango Tanzania (TBS), kwa sababu ya kutofaa kwa matumizi ya binadamu.

Shirika hilo pia limeteketeza nepi zinazotumika mara moja na kutupwa, ziitwazo Smart Baby, kwa kuwa hazikidhi viwango vya ubora vinavyotakiwa na kwa sababu zimekwisha muda wa matumizi.

Akizungumza baada ya bidhaa hizo kuteketezwa katika dampo la Pugu Kinyamwezi, nje kidogo ya Jiji la Dar es Salaam juzi, msemaji wa TBS, Roida Andusamile alisema bidhaa zote zina thamani ya Sh milioni 20.
Kwa mujibu wa Andusamile, wakati bidhaa zilizoingizwa kwa ajili ya Halmashauri ya Tarime zililetwa zitolewe msaada kwa wahitaji kwenye eneo hilo, na nepi ziliingizwa nchini ili ziuzwe.

Aliitaja kampuni iliyoingiza nepi hizo kutoka China kuwa ni Chaoming & Xlambin Chen, iliyolenga kuzisambaza katika soko la ndani na kwa faida.

Andusamile alisema, “kwa kawaida bidhaa mbalimbali zinapoingizwa nchini kutoka nje kwa ajili ya biashara, kupitia katika mipaka yetu, bandari na viwanja vyetu vya ndege hukaguliwa na maofisa wa udhibiti ubora kutoka TBS, ili kujiridhisha endapo zinafaa kwa matumizi au la”.

Alisema baada ya kukagua mizigo hiyo katika bandari ya Dar es Salaam na kupima sampuli kwenye maabara husika za shirika hilo, yalibainika mapungufu kadhaa, ikiwemo kwisha kwa muda wa matumizi.

Ofisa Udhibiti Ubora wa TBS, Salome Emmanuel alieleza kuwa, mbali ya muda wa matumizi ya nepi hizo kwisha, vipimo vya sampuli za bidhaa hiyo vilionesha kuwa hazifai kutumiwa kuvalishwa watoto, kwa sababu zina madhara kwa afya zao.

Bidhaa za msaada ambazo watu wa Marekani wanaelezwa kuchanga ili kusaidia wahitaji Tarime, ambazo hata hivyo ziliteketezwa ni losheni za watoto, sabuni za maji kwa ajili ya kunawa mikono, dawa za meno aina ya Colgate na Crest.

Nyingine ni dawa za kusukutua mdomo ili usinuke, sabuni za kuoshea nywele pamoja na sabuni za maji za kuogea. Ilielezwa kuwa bidhaa hizo zilibainika mwishoni mwa mwaka jana, na kwamba zilizoingizwa kibiashara ziliteketezwa kwa gharama za kampuni iliyoagiza huku za msaada zikiteketezwa na TBS.

0 comments:

Post a Comment