Monday, January 4, 2016



HOJA SI UKUBWA WA BARAZA, HOJA NI UKUBWA WA GHARAMA ZA KUENDESHA SERIKALI

Nimefuatilia jinsi ambavyo hoja yangu niliyoitoa juzi kwa nia njema ilivyojadiliwa nchini kwa kuungwa mkono na wengi na wengine kuipinga.
Mimi nadhani hoja yangu isijadiliwe au kukanushwa kisiasa, bali iangaliwe tu kiuhalisia ili kusaidia Serikali ya Rais Magufuli.

Aidha najua sana kwamba katibu mkuu siyo mjumbe wa baraza la mawaziri. Lakini najua vile vile kwamba jina au cheo tu cha uwaziri si kila kitu kwenye kupunguza gharama za kuendesha serikali. Gharama za kuendesha serikali ni idadi ya mawaziri, makatibu wakuu na wakurugenzi wa idara mbalimbali za serikali, na gharama zingine za kuendesha idara zao.

Na wala sijapinga mazuri anayofanya rais hadi sasa. Mbona pale rais alipofanya vizuri tumempongeza? Kwa mfano kutumbua majipu ambayo yaliivishwa tayari na serikali ya awamu ya nne. Vile vile alipopunguza idadi ya wizara na idadi ya mawaziri kutoka 29 kufikia 19 mbona tulipongeza? Na hapa tuliamini ni mwanzo wa kupunguza ukubwa na gharama za kuendesha serikali. Nasema mwanzo kwa sababu ukubwa na gharama za kuendesha serikali si kupunguza tu idadi ya wizara na mawaziri, bali kupunguza pia idadi ya makatibu wakuu ili kulingana na idadi ya wizara....ni kupunguza na kuunganisha idara mbalimbali za serikali na wakurugenzi wake. Ukifanya hivyo ndiyo unapunguza gharama za kuendesha serikali. Na hii ndiyo ilikuwa ahadi ya Magufuli kwenye kampeni. 

Lakini kama ameona kwamba kuleta ufanisi serikalini lazima ajaze watendaji wengi kwenye wizara, kama anavyoendelea kufanya, aseme tu hivyo, lakini akijua hatua hiyo haitapunguza gharama za kuendesha serikali ambazo wabunge, hasa wa upinzani, wamekuwa wakipigia kelele kwenye serikali ya awamu ya nne.

Hata hivyo hili la kuleta ufanisi pamoja na kuteua makatibu wakuu wengi wanaoonekana wazuri kwa utendaji, kuna wizara ambazo hakushauriwa vizuri na akateua makatibu wakuu wale wale na kuwarudisha pale pale wakati walikuwa "mizigo" na walikwamisha mno sekta husika katika awamu ya nne. Hawa ni watu ambao rais au katibu mkuu kiongozi angeenda kwenye wizara zao leo na kuitisha kura ya siri ya wakurugenzi na wafanyakazi wote, asilimia 90 ya watumishi wote wangewakataa makatibu wakuu hao. Ni heri kukosea kuteua kwa mara ya kwanza kuliko kukosea kuteua "mizigo" iliyokuwepo.

Tukirudi kwenye hoja ya msingi ya gharama za kuendesha serikali, nimesema na ninarudia kusema: bila kutakiwa kutoa takwimu hapa, gharama za waziri mmoja na ofisi yake ni ndogo sana kulinganisha na gharama za katibu mkuu mmoja na ofisi yake, kwani waziri tayari analipwa sehemu kubwa ya mshahara na marupurupu kutokana na yeye kuwa mbunge (na hapa niwajuze baadhi ya walionipinga kwamba waziri halipwi mishahara miwili - ya ubunge na ya uwaziri).

Na hapa hatujajadili mikanganyiko mingine ambayo haijawekwa wazi hadi sasa. Kwa mfano kutakuwa na afisa masuhuli mmoja wa wizara au maafisa masuhuli wawili au watatu kwenye baadhi ya wizara? Kwa kawaida wizara inakuwa na fungu (vote) moja; sasa katika hali hii kila idara ya wizara itakuwa na fungu (vote) tatu (ukiacha idara zinazojitegemea)? Je hili la afisa masuhuli mkuu wa wizara kutokuwepo haitaleta shida katika uwajibikaji? Na vipi katika kusimamiwa na bunge na kamati zake? Nani hasa mtendaji mkuu wa wizara atakayewajibika kwa bunge kwa mambo ya kisera ya wizara nzima? Wote watatu? 

Hatua hii ya rais magufuli ya kuwa na makatibu wakuu wa vitengo (na siyo wa wizara) ingesubiri hoja ya kikatiba ya mawaziri kutokuwa wanasiasa (wabunge) ili wawe watendaji wakuu na wawajibikaji wakuu wa wizara (cabinet secretaries) kama ilivyo nchi ya jirani ya Kenya.

Lakini kwa sasa ningeshauri hoja hii iahirishwe halafu turudi tena kuijadili baada ya "taasisi" ya makatibu wakuu wapya kupangwa - kwa maana ya kila mmoja kupangiwa idara na wakurugenzi chini yake (na ninahisi kutakuwa na nyongeza ya idara). Na baada ya hapo uchambuzi wa gharama za kuendesha serikali hii ufanywe na ulinganishwe na gharama za uendeshaji wa serikali ya mwisho ya JK ambayo tayari ilikuwa inalalamikiwa kwa ukubwa wake.

Dr. Milton Makongoro Mahanga

0 comments:

Post a Comment