Friday, August 12, 2016




Terehe 8/6/2016 Serikali kupitia Polisi ilipiga marufuku mikusanyiko au maandamano ya Vyama vya siasa nchini kwa madai ya kuwa na taarifa za kiintelinjisia za baadhi ya vyama vya siasa kutaka kuvuruga amani nchini kwa kisingizo cha Demokrasia.
Demokrasia ni mfumo wa Serikali ambao mamlaka kuu inakuwa na jukumu la kutekeleza maamuzi ya Wananchi wake aidha moja kwa moja au kupitia mfumo wa Uwakilishi, lakini yote hufanyika kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri. Kwa mujibu wa kipengele cha 5 Sheria ya Vyama vya Siasa Tanzania ya Mwaka 1992 "Chama cha siasa"  

maana yake ni kikundi chochote kinachoundwa kwa kutumia Katiba ya Chama kile kwa lengo la kushindana kuongoza Serikali, au Serikali za Mitaa katika Jamhuri ya Muungano, kwa njia ya uchaguzi ambao Wananchi kupiga kura na kuchagua Chama cha Siasa wanachokitaka kiwatawale. Katika Uchaguzi wa mwisho hapa nchini Wananchi wengi waliichagua CCM kuwaongoza tena kwa Miaka 5 ikiwa sasa tuna miezi 10 tu toka uchaguzi huo uishe, tayari kumetokea matukio mengi kutoka kwa walioshindwa uchaguzi huo wakijificha nyuma ya mgongo wa Demokrasia. Kwamba eti Serikali iliyopo madarakani sasa hivi haiheshimu Demokrasia na mara kwa mara wamekuwa wakiitishia Serikali hii kuandamana au kutumia fujo ili kuona Serikali inatumia Demokrasia katika kuishi nao yaani Wapinzani. Chokonoa chokonoa ya Wapinzani iliipelekea Serikali kupiga marufuku mikutano au mikusanyiko yote ya vyama vya siasa nchini kwa muda.

Mwenyekiti wa Chama cha Maarufu cha Upinzani nchini TLP Mh. Augustine Mrema, aliwahi kusema "Demokrasia isiyothibitiwa ni magofu. Hatupaswi kuruhusu hili kutokea katika nchi yetu ". Na kama Mwanasiasa mashuhuri Duniani Norman Mailer alivyowahi kusema “Vita vyovyote ambavyo vinahitaji wapiganaji kupoteza fahamu kwanza ndio wapigane ni vita vibovu na havifai” Mrema kama Mailer wote wapo sawa katika maoni yao ambayo, kwa hakika, yana anzisha somo muhimu katika vipengele muhimu vya mfumo wa vyama vingi na somo zima la 'elimu ya siasa,demokrasia na uhuru' katika Taifa kama letu hasa ukizingatia maneno mazito yaliyowahi kutamkwa na Mwenyekiti Mao Tsetung kwamba “Bila utafiti, hakuna haki ya kuongea”. Vyama vingi vya siasa nchini hasa vya Upinzani vimekuwa vikipingana na Serikali ya sasa kwa kisingizio cha Demokrasia ambayo kiuhalisia vinakosa hoja nzito na za msingi. Kwa mfano hata Marekani kunakoaminika kuwepo kwa Demokrasia ya kweli bado ukivaa fulana inayomsifia Bin Laden unakuwa umevunja Sheria za Taifa hilo kubwa Duniani. Rais wa zamani wa Marekani aliwahi kusema “Hakuna Demokrasia isiyokuwa na mipaka” ingawa pia wote tunajua kimsingi kwamba kazi namba moja ya Wapinzani ni kupingana na Serikali kistaarabu katika kuelekezana ili kulisaidia Taifa na sio sababu nyingine yoyote.

Tukio hili la Serikali kupiga marufuku maandamano na mikusanyiko sio geni Duniani, kwa mfano Tarehe 13/2/2015 Serikali ya Uingereza ambako tunaamini kuna Demokrasia iliyokomaa kwa miaka zaidi ya 300 kuliko yetu yenye Miaka 50 tu iliwakatalia kina Mama wa “Million Women  Raise Demonstration” kwa kuhofia vurugu kwenye maandamano hayo. Tarehe 15/4/2016 Manispaa ya Hollywood ilimkatalia kibali cha mkusanyiko mgombea urais wa Marekani kwa Chama cha Republican Donald Trump kwa sababu zile zile kama za Serikali ya Tanzania za kuepusha vurugu, Meya wa mji huo Bw. Harvath alisema Polisi wake wanazo habazi za kutosha za kiintelijisia za kupangwa kufanyika vurugu kwenye mkusanyiko huko na kwamba kipengele cha Katiba ya nchi hiyo “The First Ammendment” ambacho kinalinda matukio kama hayo bado hakina nguvu ya kuilazimisha Serikali ya Manispaa kuruhusu mkusanyiko huo. Mwaka 1949 Serikali ya Marekani ilipiga marufuku mkusanyiko au maandamano yoyote kufanyika kwenye eneo la Mahakama Kuu ya nchi inayojulikana kwa jina maarufu kama “Supreme Court”.Mwanasiasa Maarufu duniani Winston Churchhil aliwahi kusema ‘’Hoja bora dhidi ya demokrasia ni dakika tano ya mazungumzo na wapiga kura wa kawaida kwa mujibu wa Katiba ya Nchi.” 

Ikiwa na maana kwamba kama Serikali inakosea ni muhimu sana kuwepo na ukumbushwaji kutoka kwa wahusika ambao ni Upinzani lakini kwa njia ya kuheshimu Katiba ya Nchi.
Watanzania kwenye uchaguzi uliopita tulikuwa tunakubaliana kwa kauli moja kwamba tunataka mabadiliko, tulikuwa tumechoshwa kabisa ya jinsi tulivyokuwa tukijitawala huko nyuma na kwa bahati nzuri tukampata Rais Magufuli ambaye katika hotuba zake zote za Kampeni aliweka wazi dhamira yake ya mabadiliko akiwa Rais. Sasa baada ya kuwa amekuwa akijaribu sana kuliondosha Taifa kwenye matumizi yasiyokuwa na tija kama kutumia mapesa mengi sana kwa ajili ya sherehe huku wananchi wakiteseka mahospitalini na wanafunzi kukosa madawati shuleni. Pia Rais Magufuli alisitisha tabia ya kuonyesha Bunge letu asubuhi kwenye TV ya TBC na badala yake kuonyeshwa usiku kukwepa gharama ya kutumia pesa za Serikali Shillingi karibu Billioni 4 kila mwezi kwa sababu ya kuonyesha “Bunge live” tu. Katika kuhakikisha Bunge la Wananchi linaendeshwa kwa heshima na nidhamu kama Sheria ya Bunge inavyotaka, mamlaka ya Bunge imetoa adhabu nzito sana kwa Wabunge wote waliovunja Sheria hizo ambapo pia kabla ya kupewa adhabu hizo Wabunge hao waliitwa na kupewa nafasi ya kujietetea kama Demokrasia ya Dunia nzima inavyotaka. Haya yote ni mabadiliko ambayo sisi wenyewe kwa kumchagua Rais Magufuli, tulikuwa tunajua kwamba yanakuja.

Hakuna kitu kigumu katika maisha ya mwanadamu kama Mabadiliko au “Change” na hasa kama ni mabadiliko kama ya siasa yetu Tanzania ya kutoka kwenye kona ya kawaida kwenda kwenye kona mya isiyojulikana au inayojulikana kwa Rais mpya aliyechaguliwa kama wetu ambaye aliyaimba sana mabadiliko haya kwenye kampeni zake za urais. Mabadiliko ya kweli kama tuliyonayo sasa hivi hapa nchini huwa yanakuja kwa wakati muafaka kama tuliokuwa nao wakati wa uchaguzi na mabadiliko hayalazimishwi, na haijawahi kutokea Duniani mabadiliko yakawa matamu. Siku zote Mabadiliko muhimu na mazuri kwa maendeleo ya binadam huja na maumivu makubwa sana kwa wahusika yaani Wananchi. 

Na Ni jukumu sahihi la vyama vya siasa katika mazingira yetu siasa kuhakikisha kwamba vinaiweka Serikali katika mstari wa Sheria kwenye kutimiza mabadiliko haya kwa sababu historia nyingi zinaonyesha ni rahisi sana kwa Serikali kwenda nje ya mstari wa Demokrasia kwenye kuleta mabadiliko kitu ambacho bado Serikali ya Rais Magufuli haijakifanya bado pamoja na makelele mengi ya Upinzani kwamba wanaiminya Demokrasia.

Kupigwa marufuku mikutano ya vyama vya siasa inatakiwa uwepo wa 'uelewa wa siasa juu ya demokrasia na uhuru' ambayo faida yake ni nadra sana kuipata tu kutoka kwa viongozi ambao  maslahi yao ni kujenga ghasia katika nchi yetu ya amani. Demokrasia inaweza kukiukwa kwa bahati mbaya kwenye mchakato wa mabadiliko lakini huwezi kuirekebisha Serikali kwa kutumia fujo na vurugu kwa sababu Katiba inaipa nafasi Serikali kutumia vyombo vyake vya dola kuthibiti waleta vurugu.


 Katiba inatoa nafasi kwa vyama vyote husika kupiga kampeni kwa siku 60 na baada ya uchaguzi kuisha bado Katiba inatoa nafasi ya malumbano ya kisiasa kuhamia Bungeni baina ya watawala na Wapinzani. Sasa kama ukifikia kushindwa kutumia jukwaa la Bunge kujenga hoja za kuirekebisha Serikali mpaka kufikia kuvunja kanuni za Bunge na kuadhibiwa, maana yake ni kwamba aidha umefilisika kisiasa au hujui sababu ya kuwepo kwako kwenye mfumo wetu wa siasa. Demokrasia inaongozwa na Sheria na inapatikana kwa kutumia Sheria, lakini haiwezi kupatikana au kurekebishwa kwa kutumia fujo na vurugu. Fujo na vurugu kwa kutumia mgongo wa Demokrasia ni hatari kwa Taifa kwa sababu kikundi kidogo cha Upinzani kwenye Taifa kikiruhusiwa kufanya vurugu na fujo kuonyesha kutoridhishwa na nchi inavyoendeshwa ina maana ya kuwapa nafasi kundi kubwa la Chama tawala linaloliridhika na nchi invyoendeshwa kufanya fujo na vurugu kuwapinga Wapinzani. Serikali yoyote duniani haiwezi kukaa pembeni na kuruhusu ukiukwaji huu wa Demokrasia, Serikali iheshimu sheria za jamhuri na vyama vya siasa pia viheshimu Sheria mpaka sasa Serikali haijaonyesha kuvunja Sheria zake za kuheshimu Demokrasia, lakini Wapinzani wanaonekana kukosa agenda ya kisiasa kwa wananchi katika kipindi hiki cha mabadiliko tuliyoyataka wenyewe wananchi wengi wa Tanzania.

MUNGU IBARIKI TANZANIA
William Malecela aka Le Mutuz Nation Cell:- +255 717 618 997 Email:- willymalec@gmail.com

0 comments:

Post a Comment