Tuesday, August 2, 2016


TAMASHA la bendi za Tanzania lililofanyika Leaders Club Jumamosi usiku ni habari njema kwa wapenzi wa muziki wa dansi, ni mwarubaini na nuru ya kuukwamua muziki huo unaoonekana kudumaa.

Tamasha hilo lililojulikana kama Tanzania Band Festival, linapaswa kuwaamsha wadhamini ambao wamekuwa wakiwekeza nguvu nyingi kwenye muziki wa kizazi kipya ambao hutawaliwa zaidi na mfumo wa kutumia CD (Playback).

Muziki wa bendi (live) hususan ule wa dansi, ndiyo muziki wa ukweli, muziki ghali, muziki unaotoa ajira kubwa, hivyo anapotokea mwandaaji kama Q Plus umma wa wapenda dansi unastahili kushukuru na kuunga mkono hasa kutokana na ukweli kuwa ‘wawekezaji’  (mapromota) wengi hawaamini katika kuwekeza kwenye muziki wa dansi.

Q Plus walifanya kila njia kuhakikisha tamasha linanoga kuanzia usalama wa eneo la tukio, mapambo ya kisasa, sound bab kubwa na jukwaa lenye hadhi ya kimataifa …Lakini pamoja na yote hayo, pamoja na nia na dhamira nzuri ya waandaaji, yapo mapungufu kadhaa ambayo Q Plus na washirika wao wanastahili kuyafanyia kazi katika siku zijazo hasa kutokana na ahadi yao kuwa tamasha lile litakuwa likifanyika kila mwaka. Nitataja mapungufu saba niliyoyaona.


Kwanza kabisa ni kiingilio: Shilingi 15,000 kwa usawa wa leo si mchezo – unapozungumzia kiasi hicho cha pesa maana yake mtu anapaswa kuwa na pesa isiyopungua elfu 25 ili angalau aweze kuchukua usafiri wa boda boda wa kwenda na kuondoka Leaders Club, awe na uwezo japo wa kunywa chupa moja ya soda. Nadhani shilingi 10,000 ingekuwa muafaka zaidi.

Muda wa onyesho: Kutangaza kuwa onyesho lingeanza saa 5 asubuhi ilikuwa ni kosa la kiufundi, naamini wako wengi waliohofia kwenda eneo la tukio saa 2 za usiku kwa kuamini kuwa nusu ya ratiba itakuwa imewapita – onyesho lilianza saa 12 za jioni, tupunguze ushawishi usio na tija na uliopambwa na chembe chembe za uongo.

Muda wa bendi kukaa jukwaani: Hili nitaliesemea kwa urefu zaidi. Mwanzo tuliambiwa kila bendi itakaa jukwaani kwa dakika 45, lakini baadae zikapungua hadi 30 na mwishowe ikawa 20 – hii maana yake ni kwamba waandaji hawakupiga hesabu nzuri za masaa ya onyesho lao kwa kugawanya na idadi ya bendi, matokeo yake kadri muda ulivyokuwa ukienda ndivyo walivyoona kuwa ipo hatari ya bendi nyingine kukosa kabisa muda wa kupanda jukwaani – suluhisho likawa kupunguza muda katikati ya tamasha.

Hakukuwa na ulazima wa bendi zote kulingana muda wa kukaa jukwaani - QS International Band kupata dakika 45 halafu FM Academia ipate dakika 20 halikuwa jambo sahihi.

Tukubali tusikubali, katika katika tamasha lile, zilikuwepo bendi ambazo piga ua ndiyo zilikuwa chambo cha kuleta wateja wengi (crowd puller) – Nitazitaja bila woga: FM Academia, Twanga Pepeta, Msondo Ngoma, Sikinde, Yamoto Band na Malaika ya Christian Bella ambayo haikuwepo Leaders kama matangazo yalivyoashiria  – hizi zilipaswa kupewa kipaumbele katika muda wa kukaa jukwaani.

Wako watakaotaka kujua vigezo nilivyotumia kuzitaja bendi hizo kama “crowd puller”. Nitafafanua: Matokeo ya show ya Twanga na FM pale Escape One yanajulikana, matokea ya show ya miaka 37 ya Sikinde iliyosindikizwa na FM yanajulikana, matokeo ya show za mpambano wa Sikinde na Msondo yanajulikana – yote yalifana sana, moto wa Yamoto Band unajulikana.

Utitiri wa bendi: Kwa kuanzia, tamasha kama hili halikupaswa kuwa na bendi nyingi, bendi sita au saba zingetosha sana, hii ingetoa nafasi kwa bendi kutumbuiza kwa muda wa kutosha, ingepunguza gharama za onyesho na hivyo kusaidia kupungua kwa bei ya kiingilio - Wako pia mashabiki wanaokataa kwenda kwenye maonyesho yenye msururu wa bendi nyingi kwa kuhofia kuwa bendi aipendayo haitatumbuiza kwa muda mrefu – kwamba anaweza kulazimika kukaa hadi saa 9 za usiku kuisubiri bendi aipendayo na kisha ikapiga wimbo mmoja tu.

Dhumuni la tamasha halikueleweka: Wengi tulidhani ni tamasha la bendi za muziki wa dansi, lakini inavyoelekea waandaaji walijali neno “BAND” bila kujali ni bendi ya aina gani ya muziki, iwe dansi, reggae, chakacha, afro pop, haikujalisha.

Bendi kama B Band, Top Band na QS hazikuendana na dhana tuliowekewa kichwani kuwa tamasha lilikuwa maalum kwaajili ya kunyanyua muziki wa dansi - sina tatizo sana na Skylight Band ingawa huwezi kuitaja kama bendi ya dansi kwa asilimia 100, sina tatizo na Yamoto Band ambayo licha ya kukaa ki-bongo fleva, lakini wanachokifanya jukwaani ni muziki wa dansi kwa sana tu.

Promosheni: Waandaaji walipaswa kujitanua zaidi kwa kutumia vituo vingi vya radio hususan vile vinavyoutendea haki muziki wa dansi. Hili lina gharama lakini lingewezekana kama waandaji wangepunguza baadhi ya mambo ikiwemo kupunguza msururu wa bendi nyingi. Naiamini sana media iliyobeba show (Clouds Media), lakini ingependeza zaidi kama matangazo yangepenya kwenye vituo vingine vya radio na hata televisheni ikibidi.

Eneo la tukio: Kwasasa napata shaka kuamini kuwa Leaders Club ni sehemu sahihi ya kufanyia matamasha ya muziki wa dansi kulinganisha na sehemu kama TCC Club ambayo nina uhakika gharama zake ni nafuu zaidi.

0 comments:

Post a Comment