Monday, March 27, 2017


Mcheza tennis toka nchini Uingereza mwanadada Johanna Konta amefanikiwa kutinga katika hatua ya 16 bora katika michuano ya wazi ya Miami mara baada ya kumshinda Pauline Parmentier toka nchini Ufaransa.
Katika mchezo huo Konta, anaeshikilia nafasi ya 10 kwa ubora duniani alishinda kwa seti s 6-4 6-0 ndani ya dakika 63.

Kutokana na ushindi huo, sasa Konta atakutana na Lara Arruabarrena ambae alipata ushindi wa seti 7-5 7-5.
Kufanikiwa kwa Konta, 25, kufika katika hatua ya 16 bora ni mafanikio makubwa kwani katika michuano mikubwa kwa mwaka huu amekuwa akipata wakati mgumu sana toka alipotolewa katika hatua ya robo fainali katika michuano ya wazi ya Australia mwezi januari mwaka huu.

Mara baada ya kukamilika kwa mchezo huo, Konta amesema amefurahishwa sana na matokeo ambayo ameyapata kwani ilimlazimu kupigana kufa na kupona ili kupata matokeo hayo.

Katika mchezo mwingine mchezaji nambari moja kwa ubora duniani Angelique Kerber amefanikiwa kupata ushindi katika mchezo dhidi ya Shelby Rogers kwa kumtandika kwa seti 6-4 7-5.

Sasa Angelique Kerber atakutana na Mjapan Risa Ozaki, ambae amepata ushindi mbele ya Julia Goerges kw akumfunga kwa seti 7-6 (7-5) 6-3.

Kwa upande wa wanaume mchezaji mmoja mmoja Kei Nishikori toka Japan amepata ushindi wa seti 7-6 (7-2) 6-7 (5-7) 6-1 dhidi ya Mhispania Fernando Verdasco anaeshikilia nafasi ya 25 kwa ubora duniani.

Mchezaji Milos Raonic toka Canada yeye amelazimika kujitoa katika michuano hiyo kutokana na kusumbuliwa na msuli wa mkono. Milos alitakiwa kucheza dhidi ya Jared Donaldson.


Kwa upande wa wachezaji wawili wanaume, Jamie Murray pamoja na Bruno Soares waliwashinda Paolo Lorenzi na Joao Sousa kwa seti 6-0 6-3 katika mzunguko wa pili.

0 comments:

Post a Comment