Watanzania
wameombwa kujitoa kwa hali na mali ili kuiwezesha timu ya Taifa kwa vijana
wenye umri chini ya miaka 17 Serengeti Boys iweze kufanya vema katika fainali
za AFCON kwa vijana zitakazofanyika Gabon Mwezi May.
Akizungumza
na wanahabari Mwanahabari nguli nchini ambae pia ni Mwenyekiti wa KAMATI
YA HAMASA SERENGETI BOYS Charles Hilary amesema mpango uliopo ni
kuhakikisha Serengeti inamaliza katika nafasi mbili za juu katika kundi Kundi B ambalo linajumuisha timu za Angola, Mali na
Niger ili ipate nafasi ya kushiriki katika kombe la dunia kwa vijana, hivyo ni
vema watanzania wakajitoa kwa hali na mali.
Katika mkutano huo ambao ndio mkutano wa kwanza wa wajumbe wa
kamati hiyo na wanahabari toka ilivyoteuliwa na Waziri wa Habari, Utamaduni,
Sanaa na Michezo Mh Nape Nnauye, Charles ameweka wazi mipango mbalimbali ambayo
wamejiwekea ili kuhakikisha fedha inapatikana kwaajili ya kuwezesha mambo
mbalimbali yanayohitaji fedha.
Mipango hiyo ni pamoja na kuangalia uwezekano wa kuchangisha
fedha toka katika Halmashauri mbali mbali zilizopo nchini, makampuni mbali
mbali, pamoja na michango toka kwa wadau na wapenzi wa soka.
Nae Mkurugenzi wa Mahusiano wa kampuni ya Airtel Tanzania,
Beatrice Singano amesema mfumo kwaajili ya kuwawezesha Watanzania kuichangia
fedha Serengeti boys umeshakamilika na watumiaji wa mitandao yote wanaweza
kutuma fedha kwenda nambari 223344.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa Michezo nchini Yusuph Singo
ameipongeza kamati hiyo kwa yale ambayo wameyafanya hadi sasa licha ya kuwa
wamepewa majukumu hayo ndani ya kipindi kifupi.
Yusuph SIngo amewtaka pia watanzania kuchanga Fedha
bila wasiwasi kwani kamati hiyo ni kamati inayowahusisha watu waadilifu.
Katika hatua nyingine mtangazaji nguli wa habari za
michezo nchini Maulid Kitenge amesema tayari mdundo maalumu umeshaandaliwa ili
kuwawezesha wasanii mbalimbali wa muziki wakiongozwa na Msanii Diamond Plutnumz
na Alikiba ili uweze kutumika kuwahamasisha Wapenzi na wadau wa soka nchini
waweze kujitoa kwaajili ya Serengeti Boys.




0 comments:
Post a Comment