Posted by Williammalecela.com on Wednesday, March 29, 2017
 |
*LEO MACHI 29 NI KUMBUKUMBU YA KIFO CHA TX MOSHI WILLIAM*
Marehemu TX Moshi William alifariki tarehe 29 Machi mwaka 2006 siku ya
JUMATANO majira ya saa 3 asubuhi na kuzikwa siku hiyo hiyo katika
makaburi ya Keko machungwa.
Tarehe na siku ya kifo chake
vimejirudia mwaka huu na siku hiyo huwa kuna burudani ya Msondo katika
ukumbi wa Sugar Ray kwa Sokota. Marehemu TX Moshi William alijiunga na
Msondo mwaka 1982 akitokea Polisi Jazz. Miongoni mwa nyimbo alizotunga
mara baada ya kujiunga ni pamoja na Ajuza, Asha Mwanaseif, (aliomtungia mkewe), na Ashibaye.
Alitunga nyimbo nyingi lakini nyimbo zilizotia fora sana ni pamoja na
Kilio cha Mtu Mzima, Ndoa Ndoano, Piga Ua Talaka Utatoa, Ndoa ya Isihaka
Kibene, Kaza Moyo na Ajali.
Wimbo wa Ajali aliutunga baada ya
kupata ajali ya kuparamia mti wa mvinje pale Mivinjeni Desemba 16, 2005
iliyompelekea kuvunjika mguu.
Moshi William alikua chakaramu na
mbunifu wa kutunga vionjo ikiwemo mtindo ujulikanao kama Mambo
Hadharani na katika nyimbo alipenda kuchombeza vionjo vyenye kutoa raha
na kunogesha wimbo mfano utasikia "we nani", " kidogo tu..kidogo tu",
"kwanini lakini", " watoto wanachezea umeme", "dispilin", " fair play"
nk
Wakati wa uhai wake TX Moshi William alipitia katika bendi
mbalimbali za muziki wa dansi ambazo ni pamoja na Safari Trippers,
Juwata Jazz. UDA Jazz, na Polisi Jazz bendi ambayo alitokea wakati
anajiunga msondo.
Tx Moshi William alijaliwa kupata tuzo mbalimbali mfululizo za muziki kama Kilimanjaro Music Award.
Marehemu Moshi alibatizwa jina la TX, na mtangazaji mashuhuri na wa
siku nyingi aliyekuwa mtangazaji wa Radio Tanzania, marehemu Julius
Nyaisanga Uncle J. Nyaisanga alimbatiza jina hilo kutokana na tunzi zake
za uhakika. Nyaisanga alikua mtangazaji wa RTD na kisha vituo vya
utangazaji vya ITV Radio one. Jina halisi la TX ni Shaaban Mhoja Kishiwa
ingawa alikuwa akijulikana zaidi kwa jina la Moshi William TX.
Alizaliwa mwaka 1958 Korogwe mkoani Tanga.
Kwa kweli Tx Moshi William ameacha pengo na kumbukumbu isiyosahaulika
kwa wapenzi wa Msondo na ulimwengu wa muziki wa Dansi Tanzania. Tarehe
29 wana Msondo ngoma na wapenda muziki wa dansi tumkumbuke TX Moshi
William. |
0 comments:
Post a Comment