Baada ya taarifa kuzagaa katika mitandao ya kijamii kuwa Alsay ndiye aliyevunja Kundi la Yamoto Band, Mkurungenzi wa bendi hiyo Mkubwa Fella amekanusha taarifa hizo huku akidai kila msanii wa kundi hilo ameruhusiwa kufanya kazi zake binafsi.
Akiongea na Bongo5 Ijumaa hii, Fella amedai baada ya kuona biashara ya muziki wa bendi kubadilika kila msanii wa kundi hilo aliruhusiwa kufanya kazi zake binafsi.
“Wakati wanaanza wazo lilikuwa nikumtaka Aslay awashike mkono vijana wenzake ili wafike mjini na kweli wamefika mjini kila mtu anamjua Beka, Malomboso na wengine. Lakini muziki wa sasa umebadilika sana, muziki wa bendi haulipi, wasanii wakiwa kundi na mmoja mmoja malipo ni tofauti sana,” alisema Fella.
Aliongeza, “Wateja wengi ukiwaambia Yamoto Band wanatakiwa kulipwa hivi wanakimbia, lakini msanii mmoja wanaweza kumlipa mpaka milioni 5 ukija kwa kundi zima wanalialia. Kwahiyo kwa mazingira hayo sisi kama viongozi tukaona ngoja kila mtu afanye kazi kivyake ili kila mmoja anufaike na kile anachokitolea jasho,”
Fella amedai suala la mmoja kati ya msanii wa kundi hilo kukaririwa na mitandao ya kijamii akidai Aslay ndiye aliyevunja kundi hiyo sio za kweli huku akidai huwenda msanii aliyedaiwa kusema alikaririwa vibaya.
Mpaka sasa wasanii watatu wa kundi hilo wameshaachia kazi zao binafsi.
0 comments:
Post a Comment