Friday, December 11, 2015





VMM/U.80/8/Vol.I/42 11/12/2015
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

 
Ndugu zangu waandishi wa habari, Nawapongeza sana kwa namna mlivyojipambanua katika kuhakikisha mnaitumikia nchi yenu kwa kufanya kazi kwa utaalamu wa hali ya juu unaotokana na Taaluma zenu.
Umoja wa Vijana wa Chama cha Mapinduzi kwa mwendelezo ule ule wa kuhakikisha inaendelea kutoa taarifa mbalimbali za utekelezaji wa Ilani ya CCM kwa Serikali ya awamu ya tano kwa kuhakikisha yale yote tuliyowaahidi wananchi wakati wa kampeni tunayatekeleza kwa umakini na kasi kubwa.
Ndugu waandishi wa Habari Umoja wa Vijana wa Chama cha Mapinduzi tunampongeza sana Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa uteuzi mahiri na makini wa Baraza la Mawaziri aliloliteua tarehe 10/12/2015, ni Baraza dogo lakini lililokamilika katika kuhakikisha linagusa kila Sekta. Pia ni Baraza linaloakisi adhma ya Mheshimiwa Rais ya kuhakikisha anaendelea kupunguza na kubana matumizi yasiyo ya lazima.
Tumeridhishwa na uteuzi huu ambao umesheheni Mawaziri na Manaibu Waziri wenye uwezo na weledi mkubwa sana, na hatuna mashaka kwamba watafanya kazi kwa kasi na uzalendo. Lakini pia Umoja wa Vijana tumefarijika zaidi kwa Baraza hili kuwa na Vijana wengi, kwa hakika tunaiona dhamira ya dhati ya Mh. Rais Dr. John Pombe Magufuli ya kuhakikisha Tanzania inapata mabadiliko ya haraka, sote tunaamini Nguvu Kazi ya Taifa letu ni Vijana, na tuwaombe Vijana wote mliopewa nafasi na Mheshimiwa Rais mtambue kwamba kawaamini sana kwa hiyo ni mategemeo yetu hamtotuangusha.
Ndugu zangu waandishi wa Habari, Umoja wa Vijana wa CCM inachukua fursa hii kuwataka Mawaziri wote walioteuliwa watekeleze Ilani ya CCM kwa kasi ambayo ameanza nayo Mheshimiwa Rais katika maeneo mbalimbali, Changamoto ni nyingi sana na Ilani ya CCM imeainisha kinagaubaga ni mambo gani ya msingi Serikali ya awamu ya Tano inatakiwa kuelekeza nguvu zake zote ili kuhakikisha inamkwamua Mtanzania kwenye dimbwi la umaskini, lakini sisi kama wadau wa Vijana tunaomba Mawaziri husika wamsaidie Rais kutatua changamoto za Vijana ikiwemo changamoto kubwa ya AJIRA. Ilani ya Chama Cha Mapinduzi imeainisha namna gani Serikali itatatua changamoto hii, Mawaziri husika wahakikishe wanasimamia kwa nguvu zote katika maeneo yafuatayo:-

-> Kuhakikisha mchakato wa Baraza la Vijana la Taifa unakamilika ili kuwawezesha Vijana kushiriki kwa ukamilifu katika shughuli zote za Baraza la Taifa la Vijana.

-> Utengwaji wa maeneo ya Uzalishaji Mali
-> Kuziwezesha Saccoss za Vijana
-> Kuwapatia mitaji wahitimu wa Elimu ya Juu
-> Kuanzisha vituo maalum vya Vijana kila Wilaya
-> Vijana kunufaika na milioni 50 zitakazotolewa na Serikali kwa kila Kijiji.
-> Vijana kufaidika na shughuli za maendeleo
-> Mafunzo ya TEHAMA na Ujasiamali
-> Vijana kufaidika na Mifuko Hifadhi ya Jamii
Vijana kunufaika na Mapato ya kila Halmashauri

->Vijana wajasiliamali kunufaika na manunuzi ya kila Halmashauri
-> Kuondoa kero na malalamiko kuhusu ushuru na kodi zinazotozwa na Halmashauri
-> Mapambano dhidi ya Madawa ya kulevya.
Yote haya na Mengine mengi ambayo Ilani imeainisha ili kuwawezesha wananchi Kiuchumi Mawaziri husika wanapaswa kutekeleza kwa kasi na nguvu kubwa ili NGUVU KAZI hii itumike katika kuleta maendeleo ya Taifa letu.
Ndugu waandishi wa Habari Watanzania tuna kero nyingi sana zinazotukabili, Serikali itimize wajibu wake wa kuhakikisha inawawezesha wananchi Kiuchumi lakini Mawaziri wanakazi kubwa ya kuhakikisha wanaendeleza mapambano ya kubana matumizi yasiyo ya lazima ili fedha hizo zielekezwe kwenye kuboresha huduma za Kijamii, Watanzania hatutawaelewa Mawaziri wetu kama hawatofuata maagizo ya Chama cha Mapinduzi yaliyoanza kutekelezwa kwa kasi kubwa na Mhe. Rais, na hasa Vita dhidi ya Rushwa na ubadhilifu wa Mali ya Umma.
Ndugu waandishi wa Habari Mheshimiwa Rais bado anaendelea na mchakato wa uteuzi wa Mawaziri katika maeneo ambayo hayajakamilika. Tuna Imani atakamilisha zoezi hili kwa umakini na umahili kwa vigezo alivyovitumia kuwapata Mawaziri hawa waliokwishateuliwa, Mungu amuongoze ili Serikali ikamilike.

Tunawatakia kila la kheri Mawaziri wote katika kulijenga Taifa.
Mungu Ibariki Tanzania
Mungu Ibariki Afrika
KIDUMU CHAMA CHA MAPINDUZI

Egla Obed Mamoto
KATIBU IDARA YA UHAMASISHAJI, SERA, UTAFITI NA MAWASILIANO
(UVCCM)

0 comments:

Post a Comment