SERIKALI imesema itawavua nyadhifa zao Waganga Wakuu wa Mikoa na Wilaya kwa kushindwa kudhibiti ugonjwa wa kipindupindu.
Kauli hiyo ilitolewa jana na Waziri, Wizara ya Afya, Maendeleo ya
Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu, wakati wa mkutano wake na
waandishi wa habari juu ya hali ya ugonjwa wa kipindupindu nchini.
Alisema kuna haja ya kuwachukulia hatua viongozi hao kutokana na
kutumia fedha nyingi kutibu ugonjwa huo, lakini matokeo yake wameshindwa
kudhibiti. Waziri huyo alisema haiwezekani halmashauri moja inatumia
zaidi ya Sh milioni 400 na ugonjwa bado unaongezeka.
“Hawa waganga wakuu kuna haja ya kuwawajibisha, hatuwezi kuvumilia
jambo hilo,” alisema Mwalimu. Alisema mpaka sasa zaidi ya Sh bilioni
moja zimetumika kwa tiba ya ugonjwa wa kipindupindu ambapo kati ya fedha
hizo, Sh milioni 900 zimetolewa na Hazina. “Nitazungumza na Tamisemi
kuangalia ni jinsi gani ya kuwachukulia hatua kwani haikubaliki watu
waendelee kupokea mishahara kwa kushindwa kusimamia majukumu yao,”
alisema.
Mwalimu alisema fedha zilizotumika ni nyingi na kwamba zingeweza
kufanya shughuli nyingine za maendeleo kama wangedhibiti tatizo hilo kwa
wakati.
Aliagiza Machi mwaka huu, ugonjwa huo uwe umemalizika na siyo
serikali iendelee kupata hasara wakati kuna mikoa imeweza kudhibiti
kipindupindu.
Alizitaja mamlaka za mikoa na halmashauri pamoja na watendaji wake
kuendeleza juhudi za kuzuia kusambaa kwa mlipuko wa ugonjwa huo.
Aidha, Mwalimu alisema hadi sasa wagonjwa waliougua kipindupindu
wamefikia 14,608 na kati ya hao 228 wamepoteza maisha na kwamba mkoa wa
Morogoro unaongoza kwa kuwa na wagonjwa wengi. Mikoa mingine yenye
ugonjwa huo ni Mwanza, Simiyu, Manyara, Mara, Geita na Mbeya.

0 comments:
Post a Comment