Monday, January 25, 2016




MBUNGE wa Mtera, Livingstone Lusinde (CCM) anatarajia kupeleka hoja binafsi bungeni kuhusu kuanzishwa kwa bandari kavu mkoani Dodoma.

Akizungumza na waandishi wa habari mjini hapa, Lusinde alisema uwepo wa bandari hiyo, utasaidia mkoa huo kukua kiuchumi na wakazi wengi kupata ajira mbalimbali ili waweze kuondokana na umasikini.

Mbali na kukua kiuchumi, pia ni rahisi kwa nchi jirani na kila mkoa kuchukulia mizigo yake Dodoma kwa sababu mkoa huo upo katikati ya nchi.

Alisema mkoa huo unatakiwa kupewa hadhi yake kama makao makuu ya nchi ili uweze kukua kiuchumi, badala ya kuwekeza kila kitu Dar es Salaam kwa sababu bandari itaweza kuajiri waliosoma na wasiosoma na kufanya watu kukabiliana na umasikini.

“Nchi kama Rwanda, Burundi, Kongo wataweza kuchukua mizigo yao kwa urahisi, na hii itatanua shughuli za uwekezaji Dodoma na kuufanya kuwa mkoa wenye neema. Tumejenga chuo kikuu Dodoma, watu wote hawaingii chuo kwa kucheza ngoma, wanaingia kwa kusoma, sasa watasomaje wakati hawana uwezo,” alifafanua Lusinde.

Alisema wakazi wa Dodoma sio wavivu, bali ukame unawafanya kuwa na maisha magumu, lakini zikitokea fursa za uwekezaji kama huo, wataweza kuondokana na umasikini.

Lusinde akizungumzia suala la njaa mkoani humo, alisema mkoa huo unapata mvua kidogo, hali inayofanya kila mwaka kukumbwa na njaa.

Aliiomba serikali ifanye jitihada za kusaidia kilimo cha umwagiliaji ili kuondokana na ukame uliopo.
Alisema inawezekana mkoa huo ukawa wa viwanda na kimbilio kwa wananchi wa mikoa mingine, endapo hoja yake ya bandari kavu itafanikiwa.

Lusinde aliwaomba wabunge, bila kujali itikadi zao, kumuunga mkono atakapowasilisha hoja hiyo kwa maslahi ya taifa.

0 comments:

Post a Comment