Thursday, January 28, 2016




KUHAMA kwa mawaziri wakuu wastaafu kutoka chama kimoja cha siasa kwenda kingine kumezua mjadala bungeni baada ya Mbunge wa Dimani, Hafidh Ali Tahir (CCM) kutaka Serikali ifanye marekebisho ya sheria ya mafao, stahiki zao zifutwe.

Hoja hiyo ilisababisha wabunge wa upinzani akiwemo Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani, Freeman Mbowe na Mbunge wa Vunjo, James Mbatia (NCCR Mageuzi) kumjibu Tahir kwa nyakati tofauti kupitia maswali ya nyongeza wakimshutumu kuwa ni mchochezi na hajui Katiba.

Akijibu swali la Tahir, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora), Angela Kairuki alisema kujiunga na chama chochote au kujihusisha na masuala ya kisiasa ni haki ya kikatiba ambazo haziwezi kuzuiwa au kuingiliwa.

Katika swali lake, Tahir alisema kumekuwa na tabia ya baadhi ya wanasiasa hususani mawaziri wakuu wastaafu ambao wameaminiwa na kuchaguliwa na wanachama wa chama fulani, lakini baada ya kupata madaraka huhama vyama na kwenda kunufaisha vingine.

“Je, Serikali haioni kuwa umefika wakati sasa wa kufanyia marekebisho sheria husika ili kufuta stahiki za mawaziri wakuu wastaafu wanaohama vyama vyao kwa kuwa stahiki hizo zilitokana na nguvu za chama alichohama. “Na kwamba kuendelea kumpa stahiki hizo ni sawa na kuwakejeli na kuwadharau wananchi waliomchagua?” Alihoji Tahir.

Waziri alifafanua kuwa mawaziri wastaafu wanahudumiwa kwa mujibu wa Sheria ya Mafao kwa hitimisho la kazi viongozi, Namba 3 ya mwaka 1999. Alisema sheria haielezi hatua zinazopaswa kuchukuliwa kwa Waziri Mkuu mstaafu atakayeamua kuhamia chama kingine cha siasa tofauti na chama kilichomweka madarakani na kumwezesha kushika wadhifa wa Waziri Mkuu.

“Mbali na sheria hiyo kutoweka zuio lolote kwa viongozi wa kitaifa wastaafu kujiunga na chama kingine cha siasa, Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 inalinda haki za msingi za binadamu ikiwemo haki ya uhuru wa mtu kujihusisha na masuala ya kisiasa,” alisema.

Mbowe ambaye ni Mbunge wa Hai alimshukuru Naibu Waziri kwa majibu aliyotoa huku akisema tatizo si la mbunge aliyeuliza pekee bali ni la nchi nzima. Kuhusu shutuma kwa watumishi wa umma kwamba hawatendei haki vyama vingine, waziri alisema watumishi wanatambua vipo vyama vingi na ipo ilani ya CCM ambacho ndicho chama tawala. Alisisitiza wanachotakiwa kufanya ni kutekeleza sera za serikali.

0 comments:

Post a Comment