MADIWANI na watumishi katika Halmashauri ya Wilaya ya Namtumbo mkoani
Ruvuma, wametakiwa kufanya kazi kwa ushirikiano, badala ya `kupiga
majungu.
Ushauri huo umetolewa hivi karibuni na Mkuu wa Wilaya ya Namtumbo,
Chande Nalicho wakati akitoa salamu za serikali katika kikao cha kawaida
cha baraza la madiwani ambacho kilipitia taarifa mbalimbali za
utekelezaji wa maagizo na ya serikali kuu, serikali za mitaa na
utekelezaji wa miradi yote ya maendeleo.
Alisema madiwani na watumishi wanapaswa kushirikiana kwa lengo la
kuwatumikia wananchi bila ya ubaguzi, ili waweze kufaidi mipango mizuri
ya maendeleo iliyopo katika mipango ya Serikali ya Awamu ya Tano.
Alisema kwa kuwa uchaguzi umeshapita na viongozi wa halmashauri
wameshapatikana, hakuna ulazima wa kuendeleza visa au kinyongo miongoni
mwa madiwani na watumishi, bali kuanza kuwatumikia wananchi kwa kasi.
Mkurugenzi wa Halmashauri hiyo, Ali Mpenye ameziagiza kamati za
maendeleo za vijiji, mitaa na kata kuhakikisha zinasimamia vyema fedha.

0 comments:
Post a Comment