MAMLAKA ya Mapato Tanzania (TRA) imewataka wananchi kutoa ushirikiano
kwa kutoa taarifa za maofisa wanaofanya kazi kinyume na maadili.
Akizungumza Dar es Salaam jana, Mkurugenzi wa Huduma na Elimu kwa
Mlipakodi, Richard Kayombo alisema TRA ina idara maalumu ijulikanayo
kama Idara ya Mambo ya Ndani ya TRA ambayo inashughulika na kufuatilia
maadili ya watumishi wa sekta hiyo nchi nzima.
“Tunawaomba wananchi kushirikiana na Idara ya Mambo ya Ndani ya TRA
kwa kuwapa taarifa juu ya maofisa wa TRA wanaokwenda kinyume na Maadili
ya Utumishi wa Umma,” alisema Kayombo.
Aliongeza kuwa, wananchi wanaweza kutoa taarifa kwa kupiga simu kwa
namba 0689 122 515 au kwa kutuma ujumbe mfupi kwa simu namba 0689 122
516 na kuwahakikishia kuwa taarifa zao zitakuwa zimefika sehemu husika
na zitafanyiwa kazi.
Aidha, amewatoa hofu wananchi kuwa namba hizo ni za siri na hakuna
mwananchi atakayepata tatizo lolote kwa kutoa taarifa za maofisa wasio
na maadili.
Alisema kupitia idara hiyo, TRA imepokea malalamiko mengi na
kuyafanyia kazi na kuongeza kuwa, tayari baadhi ya watumishi wamefukuzwa
kazi na wengine kupewa adhabu kali.

0 comments:
Post a Comment