Thursday, January 28, 2016




MTANDAO wa Wasanii Tanzania (Shiwata) umeamua kumpa uanachama wa heshima mchezaji bora wa Afrika kwa wachezaji wa ligi za ndani, Mbwana Samatta pamoja na kumzawadia ekari tano za ardhi katika kijiji cha Wasanii Mwanzega, Mkuranga kwa ajili ya kuanzisha Chuo cha Mafunzo ya soka.

Mwenyekiti wa Shiwata, Cassim Taalib alisema jana kuwa kikao cha Kamati Utendaji ya Mtandao huo kilichoketi juzi kilifikia uamuzi huo baada ya kufuatilia kwa karibu mafanikio ya Samatta akiwa na timu ya Taifa ya Tanzania ‘Taifa Stars’ na klabu yake ya TP Mazembe ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) na kufanya vizuri katika mashindano ya Afrika hadi kuchaguliwa kuwa mchezaji bora.

Alisema Shiwata inatoa kiwanja hicho kama zawadi kwa mchezaji huyo kutokana na uwezo wake wa kulitangaza taifa katika medani ya kimataifa katika mchezo wa soka ambako wengine watafuata nyayo zake.

Taalib alisema taratibu za makabidhiano zinafanywa kwa mawasiliano na baba yake mzazi, Ali Samatta na atakabidhiwa eneo hilo mara baada ya kurudi kutoka Ubelgiji ambako anaenda kusaini mkataba na timu ya KRC Genk ya Ligi Kuu ya Ubelgiji.

Shiwata yenye wanachama zaidi ya 8,000 inamiliki ekari 300 za kujenga makazi, kumbi za starehe, viwanja vya michezo na nyumba za kuishi katika kijiji cha Mwanzega wilayani Mkuranga na ekari 500 eneo la Ngarambe kwa ajili ya kilimo.

0 comments:

Post a Comment