WABUNGE wamesema kasi ya utendaji ya Serikali ya Awamu ya Tano
inayoongozwa na Rais John Magufuli, inatoa mwanga wa kuiwezesha nchi
kufikia Dira ya Maendeleo ya Taifa (2020-2025) baada ya miaka kumi.
Hata hivyo, baadhi ya wabunge wamesema pamoja na mafanikio yanayoanza
kuonekana, hasa matumizi ya vitendo ya kauli ya “Hapa Kazi Tu”,
kumekuwa na baadhi ya dosari, wakidai serikali haizingatii sheria,
kanuni na utaratibu katika baadhi ya uamuzi.
Waliyasema hayo wakichangia katika mjadala wa Bunge wa juzi jioni,
mjini Dodoma. Mbunge wa Sikonge (CCM), Joseph Kakunda alisema matumaini
ya sasa ya watanzania ni makubwa na baada ya miaka 10 nchi itakuwa
imepiga hatua kubwa na kuufikia dira ya maendeleo ya mwaka 2020-2025.
Alisema hilo linawezekana kutokana na Rais Magufuli kuanza kuboresha
huduma za kijamii na kudhibiti matumizi yasiyo ya lazima, jambo ambalo
linaashiria matokeo makubwa katika kupunguza umaskini.
Mbunge Anna Lupembe (Viti Maalumu -CCM), alisema Rais Magufuli
amefanya kazi kubwa hasa kwa kutumbua majipu makubwa ya watu ambao
walikuwa hawalipi kodi na matokeo yameonekana.
Pia alitaka ifike wakati maeneo ya wakulima na wafugaji yaainishwe
ili kuondoa migogoro ya mara kwa mara sambamba na kuimarishwa kwa njia
ya reli.
Naye Mbunge wa Mpanda Mjini, Selemani Kapufi (CCM) amewataka
wabunge kutokuwa walalamikaji juu ya changamoto za sera ya elimu bure
inayotekelezwa na serikali, kwani kwa kufanya hivyo watakuwa ni sehemu
ya tatizo.
Pia alitaka serikali kuunganisha kwa lami mikoa ya Katavi, Kigoma na
Tabora ili wakulima waweze kuuza mazao yao kwa wakati. Mbunge wa Babati
Mjini, Cecilia Parreso (Chadema), alisema Serikali ya Rais Magufuli
imekuwa ikiongozwa na kaulimbiu ya hapa kazi tu, lakini haizingatii na
kufuata sheria, kanuni na taratibu.
Alisema Rais anapomfukuza mtumishi wa umma taratibu za kiutumishi
zinatakiwa kufuatwa pia alisema anashangazwa fedha za elimu bure
zilizotolewa na serikali kutopata idhini ya Bunge. “Mnapeleka fedha kwa
bajeti ipi? Alihoji mbunge huyo.

0 comments:
Post a Comment