BAADA ya wakulima wa mirungi wilayani Same kupuuza agizo la kung’oa
zao hilo, Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa wa Kilimanjaro, inajipanga
kufanya kampeni ya kushitukiza kufyeka na kuwakamata wakulima wa zao
hilo katika vijiji 28 kata 13 zinavyolima zaidi hilo wilayani hapa.
Pamoja na hilo, Polisi mkoa imemkamata na kumfikisha mahakamani
Diwani wa Kata ya Pasua Manispaa ya Moshi, Charles Mkalakala kwa tuhuma
za kuizuia isikamate watuhumiwa wa uuzaji na usafirishaji wa mirungi.
Mkuu wa Mkoa huo, Amos Makalla amesema kamati yake inaandaa kampeni
maalumu ndani ya siku tano kuanzia sasa ili kutokomeza kilimo hicho
kinachotishia nguvu kazi ya vijana.
Akizungumza katika kikao maalumu cha Kamati ya Ulinzi na Usalama Mkoa
wilayani Same kuhusu “Operesheni Mirungi Same,” na kushikirikisha
vyombo vya ulinzi na usalama, madiwani, watendaji wa kata na vijiji,
Makalla alisema katika mashamba 921 yaliyotakiwa kufyekwa ni mashamba
313 yaliyofyekwa sawa na asilimia 34 tu.
Katika kikao hicho ambacho pia kiliwashirikisha wenyeviti wa vijiji
na wakuu wa vituo vya polisi, Makalla alisema serikali haiwezi kuvumilia
kuwepo kwa mashamba hayo huku wananchi wakikaidi maagizo halali ya
serikali.
“Baada ya siku tano kuanzia leo kamati yangu imejipanga kufanya
operesheni kabambe ya kuhakikisha mashamba yote yaliyobaki yanafyekwa na
wananchi watakaokaidi kutekekeza katika siku tano watakamatwa na
kufunguliwa mashitaka na kwa mujibu wa sheria ya dawa za kulevya adhabu
yake ni kifungo cha miaka hadi miaka 30 jela,” alieleza mkuu wa mkoa.
Aidha, mkuu wa mkoa ameagiza watendaji, madiwani na wakuu wa vituo
vya polisi kuhamasisha wananchi kutumia siku tano kufyeka na kung’oa
mirungi yote kabla sheria haijafuata mkondo wake.

0 comments:
Post a Comment