Sunday, January 10, 2016


 

UCHAGUZI wa mameya katika Manispaa za Ilala na Kinondoni jijini Dar es Salaam ni wa vuta nikuvute na sasa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI), George Simbachawene ameingilia kati.

Waziri huyo amemwagiza Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Said Meck Sadik kuhakikisha kabla ya Januari 16, mwaka huu uchaguzi wa mameya katika manispaa hizo, uwe umefanyika. Simbachawene alisema hayo jijini Dar es Salaam jana wakati akizungumza na waandishi wa habari.

Alisema hadi leo uchaguzi wa mameya katika manispaa hizo, umeshindwa kufanyika kutokana na sababu mbalimbali, ikiwemo kuwepo kwa mvutano wa vyama vya siasa juu ya uhalali wa wajumbe, wanaotakiwa kushiriki katika kupiga kura; na mapingamizi kadhaa ya kisheria mahakamani.

Aidha alisema kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 na Katiba ya Zanzibari ya mwaka 2010, muundo wa serikali za mitaa Zanzibar na Tanzania Bara, si jambo la Muungano.

Simbachawene alisema sheria za serikali za mitaa, zimebainisha kuwa wabunge wa viti maalumu kuwa wajumbe wa baraza la madiwani la halmashauri za wilaya; na sheria hizo zinaruhusu wabunge wa viti maalumu wa Bunge la Jamhuri ya Muungano kuingia na kuwa wajumbe wa baraza la madiwani kwenye mamlaka za serikali za mitaa katika ngazi ya wilaya.

“Kwa kuzingatia vifungu hivi vya sheria za serikali za mitaa, wabunge wa viti maalumu wanakuwa wajumbe wa baraza la madiwani kwa misingi ya mapendekezo ya vyama husika, lakini lazima mchakato wa kupatikana kwao, uwe ulianzia kwenye mamlaka hiyo ya serikali za mitaa kwa mfano wilaya, mji, manispaa au jiji husika,” alisema.

Alisema kutokana na maelezo aliyoyatoa, kwa namna yoyote ile, haiwezekani kwa mbunge au mbunge wa viti maalumu kupiga kura nje ya halmashauri ya wilaya aliyokuwepo, wakati anapendekezwa na chama chake ili kupata nafasi ya uongozi.

“Napenda kuviasa vyama vya siasa kuheshimu sheria zilizopo ili kujenga, kukuza na kudumisha demokrasia, lakini pia kuondoa na kuepusha migogoro na mivutano isiyo ya lazima baada ya kumalizika kwa uchaguzi mkuu wa 2015,” alisema Simbachawene.
Uchaguzi waahirishwa tena Agizo hilo la Waziri, limekuja baada ya uchaguzi wa mameya, uliotakiwa kufanyika jana, kuahirishwa kutokana na pingamizi, lililowekwa mahakamani kuhusu kuzuiwa kwa uchaguzi huo.

0 comments:

Post a Comment