Friday, January 22, 2016




MKUU wa Mkoa wa Shinyanga, Ally Rufunga ameliagiza Jeshi la Polisi kuwakamata na kuwahoji Mtendaji wa kijiji cha Kimandaguli na wa kata ya Lyabukande, kwa kushindwa kuzuia kutoroshwa kwa mwanafunzi aliyefaulu kuendelea na masomo ya kidato cha kwanza.
Aidha, ameagiza kukamatwa kwa watu wengine waliowezesha kutoroshwa kwa mwanafunzi huyo mwenye umri wa miaka 14, kutoka katika kijiji cha Kimandaguli na kata ya Lyabukande vilivyo katika halmashauri ya wilaya ya Shinyanga.
Agizo hilo limekuja baada ya Mkurugenzi John Myola wa Asasi isiyo ya Serikali ya Agape, inayojishughulisha na upingaji wa mimba za utotoni mkoani hapa, kutoa taarifa ya kutoroshwa mwanafunzi huyo kwenye kikao cha wadau wa elimu kilichofanyika jana.
“Jeshi la Polisi lisimamie kesi ya yule aliyetorosha mtoto wa miaka 13 huko wilayani Kishapu na kukimbilia mkoani Tabora, tunachotaka mkoa uwaondoe wanaowapa wanafunzi mimba, kuwaozesha au kutorosha wenye umri mdogo kwa kuwachukulia hatua za kisheria ikiwa ni pamoja na kuhakikisha wanaondoka mkoani humu,”Rufunga alisema.
Myola alisema, awali alipata taarifa ya simu ya mzazi wa mtoto huyo, Pauline Maximillian kuwa mtoto wake aliyekuwa amekwenda kisimani kuchota maji alichelewa kurudi na kuelezwa na watu baada ya kuanza kumfuatilia kuwa alikuwa amechukuliwa na vijana wawili.
Alisema kuwa, baada ya kupewa taarifa hiyo alimshauri mzazi huyo akatoe taarifa kwenye uongozi wa Kata, Kijiji na Polisi, na kwamba pamoja na kufanya hivyo hakufanikiwa kumpata mtoto wake hadi leo kwa sababu hakupewa ushirikiano wa kutosha kutoka kwa viongozi hao wa Kata na Kijiji. Myola alisema, “Mimi ni shahidi kwa sababu niliongea nao wote kwa njia ya simu kuhusu tukio hilo ili walifuatilie na kuhakikisha mtoto huyo anapatikana, lakini hilo halikufanyika na mzazi hakupewa ushirikiano unaotakiwa huku taarifa zikisambaa kwamba alitoroshwa na vijana wawili wa kijiji cha jirani”.
Alisema, mwanafunzi huyo alitoroshwa kabla ya matokeo wakati mzazi wake anataka apatikane ili aende shule, kwa kuwa amefaulu kujiunga na kidato cha kwanza. Inaelezwa kuwa mwanafunzi huyo alichaguliwa kujiunga na shule ya sekondari Lyabukande ambako alipaswa kuwa ameripoti kuanza masomo tangu Januari 11.
Kuhusu kesi ya watuhumiwa wa kumuozesha mtoto wa miaka 13, wilayani Kishapu, Myola alisema, Polisi inatuhumiwa kubadili jina na maelezo ya mtuhumiwa aliyetoroka naye huku tayari asasi hiyo ikiwa na rekodi nzima ya maelezo ya kwanza yaliyotolewa siku aliyokamatwa.

0 comments:

Post a Comment