MKUU wa Mkoa wa Dar es Salaam, Said Mecky Sadiki amewataka wananchi
waliobomolewa nyumba zao katika maeneo ya mabondeni na kukaidi kuhama
kwa kuendelea kuishi kwenye vifusi, wahame wenyewe kwa hiari kabla ya
kuondolewa kwa nguvu na Jeshi la Polisi.
Pamoja na hayo, Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA), imeendelea
kutoa tahadhari kwa Watanzania katika mikoa mbalimbali ikiwemo mikoa
inayopata mvua mara moja na ile inayopata mara mbili kwa mwaka kutokana
na mvua zinazoendelea kunyesha.
Akizungumza na gazeti hili kwa simu jana, Sadiki alisema kitendo cha
wananchi hao kuendelea kuishi katika maeneo hayo ya bondeni huku mvua
zikiendelea kunyesha ni hatari kwa maisha yao na ni sawa na kutaka
kujiua.
“Nawataka waondoke wenyewe kwa hiari yao kwani usalama wa maisha yao
uko mikononi mwao, kuendelea kuishi katika maeneo yale ni hatari kwao na
watoto wao, lakini kama Serikali hatutakaa kimya na kuona wananchi wetu
wakihatarisha maisha yao, tutawaondoa kwa nguvu wakikaidi,” alisema.
“Tunatumia Polisi kwa sababu kitendo cha wao kubaki kwenye eneo la
hatari kama hilo la bondeni huku mvua kubwa ikiendelea kunyesha ni sawa
na mtu anayetaka kujiua. Kutaka kujiua ni kosa, sasa sisi tutafanya kama
vile tumewakuta hawajajiua tutawakamata kwa nguvu na kuwaondoa pale,”
alisisitiza.
Gazeti hili lilishuhudia zaidi ya familia 12 zikiwa zimejijengea juu
ya vifusi vibanda chakavu vya mabati na kuendelea kuishi katika bonde la
Mkwajuni katika eneo ambalo tayari nyumba zilizokuwapo zimebolewa.
Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Rukwa, Magalula Said Magalula
alisema pamoja na kwamba mkoani humo mvua zinaendelea kunyesha kwa kasi,
hakuna madhara makubwa yaliyojitokeza isipokuwa uharibifu mdogo wa
madaraja, baadhi ya nyumba kuezuliwa mapaa na maji kufurika kwenye mito.
Akizungumzia utabiri wa hali ya hewa katika kipindi hiki, Mkurugenzi
Mkuu wa TMA, Agnes Kijazi, alisema tayari mamlaka hiyo ilishafafanua
kuwa katika maeneo yanayopata mvua mara moja kwa mwaka, yataendelea
kupata mvua.
0 comments:
Post a Comment