Friday, January 8, 2016




WIZARA ya Fedha na Mipango imetoa onyo kwa wakuu wa shule za msingi na sekondari watakaotumia ovyo Sh bilioni 18.77 zilizotolewa na serikali kwa ajili ya kutoa elimu bure.

Katika kuhakikisha fedha hizo zinatumika ipasavyo, wahusika wametakiwa kuweka wazi fedha walizopokea kutoka serikalini ili wananchi wafahamu alichopewa mhusika na matumizi yake.

Bodi za shule zimepewa kazi ya kuhakikisha zinasimamia matumizi ya fedha hizo na kutoa taarifa kwa atakayebainika kutumia fedha hizo vinginevyo ili ashughulikiwe.

 Waziri wa Fedha na Mipango, Dk Philip Mpango alitoa maagizo hayo jana wakati akizungumza na waandishi wa habari kuhusu mapato na namna Serikali ya Awamu ya Tano ilivyovunja rekodi katika ukusanyaji.

Aliwataka pia wakuu wa wilaya, mikoa na wakurugenzi wote nchini kusimamia fedha hizo ambazo Sh bilioni 14.7 zimepelekwa kwenye shule na Sh bilioni tatu zimepelekwa katika vyombo vya usimamizi wa mitihani.

Akizungumzia ukusanyaji wa mapato, Dk Mpango alisema Desemba mwaka jana walifikia Sh trilioni 1.592 ikiwa ni nyongeza ya asilimia 18.9 ya lengo la mwezi huo. Alisema lengo la kukusanya mapato ya ndani kwa mwezi huo ilikadiriwa kuwa Sh trilioni 1.338 huku mwaka 2014 mwezi kama huo zilikusanywa Sh trilioni 1.104 ongezeko ambalo ni asilimia 44.2.

0 comments:

Post a Comment