WIZARA ya Fedha na Mipango imetoa onyo kwa wakuu wa shule za msingi
na sekondari watakaotumia ovyo Sh bilioni 18.77 zilizotolewa na serikali
kwa ajili ya kutoa elimu bure.
Katika kuhakikisha fedha hizo zinatumika ipasavyo, wahusika
wametakiwa kuweka wazi fedha walizopokea kutoka serikalini ili wananchi
wafahamu alichopewa mhusika na matumizi yake.
Bodi za shule zimepewa kazi ya kuhakikisha zinasimamia matumizi ya
fedha hizo na kutoa taarifa kwa atakayebainika kutumia fedha hizo
vinginevyo ili ashughulikiwe.
Waziri wa Fedha na Mipango, Dk Philip
Mpango alitoa maagizo hayo jana wakati akizungumza na waandishi wa
habari kuhusu mapato na namna Serikali ya Awamu ya Tano ilivyovunja
rekodi katika ukusanyaji.
Aliwataka pia wakuu wa wilaya, mikoa na wakurugenzi wote nchini
kusimamia fedha hizo ambazo Sh bilioni 14.7 zimepelekwa kwenye shule na
Sh bilioni tatu zimepelekwa katika vyombo vya usimamizi wa mitihani.
Akizungumzia ukusanyaji wa mapato, Dk Mpango alisema Desemba mwaka
jana walifikia Sh trilioni 1.592 ikiwa ni nyongeza ya asilimia 18.9 ya
lengo la mwezi huo. Alisema lengo la kukusanya mapato ya ndani kwa mwezi
huo ilikadiriwa kuwa Sh trilioni 1.338 huku mwaka 2014 mwezi kama huo
zilikusanywa Sh trilioni 1.104 ongezeko ambalo ni asilimia 44.2.

0 comments:
Post a Comment