RAIS John Magufuli amekataa na kusitisha uhaulishaji wa ardhi ya
kijiji cha Mlilingwa, tarafa ya Ngerengere wilayani Morogoro yenye
ukubwa wa ekari 3,502.
Ardhi hiyo ilitolewa kwa mwekezaji Oxford Development Limited na
hatua hiyo inatokana na kubaini kuwepo kwa mianya ya udanganyifu wakati
wa mchakato.
Kutokana na udanganyifu huo, Rais ameamuru kurejesha ardhi hiyo kwa wananchi ili itumike kwa manufaa ya wanakijiji wote.
Mgogoro wa ardhi kati ya wanakijiji cha Mlilingwa na mwekezaji huyo
ulimlazimu Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, William
Lukuvi kufika kijijini hapo ili kuhakikisha mchakato wa umilikishaji
kama ulifuata taratibu .
Akizungumza na wananchi kijijini hapo, alisema baada ya Rais kupitia
muhtasari wa kikao kilichofanyika cha kumpa mwekezaji Oxford Development
Ltd shamba hilo aligundua ulifanyika udanganyifu mkubwa uliofanywa na
viongozi wa vijiji, wilaya na idara ya ardhi na kuamuru shamba
lirudishwe kwa wananchi.
Aliwaagiza viongozi wa kijiji cha Mlilingwa, kuchukua hatua kwa
waliohusika kumpa mwekezaji shamba la ekari 3,502 kukamatwa na kuhojiwa
na vyombo vya dola kutokana udanganyifu huo.
Pamoja na kutoa agizo kwa Serikali ya Kijiji, pia aliagiza Jeshi la
Polisi na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) kuwakamata
viongozi wote, mwekezaji wa shamba hilo na waliohusika kughushi nyaraka
hata kama viongozi wameshastaafu.
Alisema hatua hiyo ni kuwezesha watu hao kuhojiwa na kuchukuliwa
hatua za kisheria kwa kudanganya serikali iwe fundisho kwa wengine
wanaofanya hivyo. Waziri alisema ametumwa na Rais kutumbua jipu hilo
alilolikuta mezani mwake, hivyo wote waliohusika ni budi wakamatwe na
kuhojiwa na mwishowe wapelekwe mahakamani.
“Nimeagizwa na Rais kuja kutumbua jipu hili na wote waliohusika
wakamatwe na wale wanaofanya udanyifu kama huu mwisho wao umefika sasa,”
alisema Lukuvi.
Kwa mujibu wa Waziri huyo, hivi sasa hakuna mkutano wowote wa kijiji
ambao utakaa na kumpitisha mwekezaji kupata shamba bila kuhudhuriwa na
Mkuu wa Wilaya, ambaye ndiye atakayepeleka barua ya maombi ya mwekezaji
kwake ikiwa na muhtasari wa kikao na saini halali za wananchi ndipo
akijiridhisha atapeleka ombi hilo kwa Rais.
Katika mkutano huo, kampuni ya Oxford Development Limited
iliwakilishwa na Kashoka Panga ambapo baada ya kujiridhisha kuwa
utaratibu ulikiukwa, waziri akatoa maagizo hayo.
Kwa upande wake, Mbunge wa Jimbo la Morogoro Kusini Mashariki, Omary
Mgumba, alisema serikali ya sasa imepania kufanya kazi kwa vitendo zaidi
na hivyo wananchi wanapaswa kuunga mkono kwani matatizo mengi
yatafanyiwa kazi.

0 comments:
Post a Comment