Wednesday, January 13, 2016


 

Mkurugenzi wa Mashitaka (DPP) ameamua kukata rufaa Mahakama Kuu dhidi ya kesi ya uchochezi inayomkabili mwanaharakati wa Kiislamu Shehe Ponda Issa Ponda.

Mwanasheria Mwandamizi katika ofisi ya DPP, Bernard Kongola amesema kuwa Serikali inapinga kuachiwa kwa Shehe Ponda ambaye alishitakiwa kwa makosa ya uchochezi katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Morogoro.

“Tayari tumeomba tupatiwe nakala ya hukumu pamoja na nyaraka za mwenendo wa shauri hilo ili upande wa mashitaka tuweze kuandaa rufaa yetu Mahakama Kuu,” alisema.

Kwa mujibu wa mwanasheria huyo, tangu waombe kupatiwa nakala ya hukumu hiyo katika mahakama hiyo ya hakimu mkazi, hakimu ambaye alikuwa anasikiliza kesi hiyo bado hajawapatia upande wa mashitaka hukumu ambayo imechapwa.

“Hatujui kuna tatizo gani, maana tunapoomba kupatiwa nakala ya hukumu, hakimu amekuwa anatuambia kwamba bado hawajamaliza kuichapa, kwa kweli hii inashangaza,” alisema.

Novemba 30 mwaka uliopita, Hakimu Mkazi wa Mahakama ya Morogoro, Mary Moyo alimwachia huru Shehe Ponda kwa maelezo kuwa upande wa mashitaka ulishindwa kuthibitisha pasi shaka yoyote mashitaka dhidi ya mwanaharakati huyo wa Kiislamu.

0 comments:

Post a Comment