MBUNGE wa Nkasi Kaskazini, Ally Kessy (CCM), ametaka kuharakishwe
kuundwa kwa Mahakama ya Mafisadi na pia kupunguzwa kwa majimbo ya
uchaguzi, kwani wabunge wamekuwa wengi bungeni.
Akichangia mjadala wa hotuba ya Rais juzi bungeni mjini hapa, Kessy
alitaka pia mbio za Mwenge wa Uhuru zifutwe kwa maelezo kuwa zimekuwa
zikiigharimu Serikali fedha nyingi.
“Majimbo yamekuwa mengi, wabunge nao ni wengi hali inayofanya
Serikali kutumia fedha nyingi kuendesha Bunge,” alisema mbunge huyo huku
akipendekeza vikao vya bajeti vyote vifanyike wilayani ili kupunguza
matumizi ya fedha za Serikali, kwa maelezo kuwa watumishi wamekuwa
wakijazana Dar es Salaam kutoka mikoa mbalimbali na kulipwa posho kwa
ajili ya kwenda kuandaa bajeti.
Alipendekeza pia kuwa kuanzia sasa bajeti ifanyike wilayani kwa
mitandao tu, kwa kuwa inatosha. Alizungumzia pia sherehe na kusema kuwa
zinafanyika za gharama kubwa kama ilivyo kwa nchi za Kiarabu.
Kadhalika, Kessy alitaka kuangaliwa kwa suala la watumishi wa huduma
za meli kwakuwa hawana likizo wala bima, huku mishahara yao ikiwa duni
na wanapostaafu hawapewi chochote. Mbali na hayo, Mbunge huyo alitaka
apewe kibali cha kufanya ukaguzi nyumba kwa nyumba akieleza kuwa mbolea
nyingi imekuwa haifiki kwa wakulima.
“Simwamini Mkuu wa Wilaya, Kamanda wa Polisi wala nani. Mwigulu
(Nchemba – Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi) nipe kibali nikakague
kijiji kwa kijiji kama mbolea inafika kwa wakulima,” alisema.
Kwa upande wake, Mbunge wa Lupa, Victor Mwambalaswa (CCM)
alimfananisha Rais John Magufuli kama Yohana Mbatizaji kutokana na kazi
anazoendelea kutenda. Huku akinukuu kitabu cha Biblia, alisema Rais
amejitoa kutumikia Watanzania sambamba na kuwawajibisha viongozi
wanaotumia vibaya madaraka na mali za umma.
Mbunge wa Viti Maalumu, Munde Tambwe (CCM) aliwataka wanasiasa kuacha
kuwatisha Watanzania kwa kuingiza maneno ya jazba juu ya hali ya
kisiasa ya Zanzibar kuwa hapakaliki ilhali si kweli.

0 comments:
Post a Comment