Monday, December 21, 2015




SERIKALI imekwishatenga kiasi cha sh. bilioni 137 kwa ajili ya kugharamia utoaji wa elimu ya bure kuanzia Januari hadi Juni, mwakani.

Kauli hiyo imetolewa jana jioni (Jumapili, Desemba 20, 2015) na Waziri Mkuu Kassim Majaliwa wakati akizungumza na mamia ya wananchi waliofika kumsikiliza kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye uwanja wa uwanja wa mikutano wa Likangala wilayani Ruangwa, mkoani Lindi.

“Kazi ya utumbuaji majipu imezaa matunda kwani tumeweza kupata fedha za kugahrimia elimu ya bure ambayo iliahidiwa na Mheshimiwa Rais John Pombe Magufuli wakati wa kampeni. Fedha hiyo tunayo, na tumeshaanza kuisambaza kwa sababu tunataka shule zikifunguliwa Januari, 2016 watoto waanze kufaidika,” alisema huku akishangiliwa.

“Atakayezigusa fedha hizi na kuzitumia vibaya ni lazima tutamtumbua tu! Tumeshawapa maelekezo Wakurugenzi wa Halmashauri pamoja na Maafisa Elimu wao na kuwaonya kuhusu matumizi ya fedha hizo,” alisema.

“Hatuhitaji mwanafunzi achangishwe hela ya mitihani, na zile shilingi 10,000/- kwa ajili ya wanafunzi wanaosoma Sekondari nazo pia tutazipeleka. Na huu ni mpango wa dharura ambao haukuwemo katika bajeti ya mwaka 2015/2016, kwa hiyo tutalazimika kuziombea kibali,” alisema.

0 comments:

Post a Comment