Friday, January 22, 2016

Waziri wa Maji na Umwagiliaji, Gerson Lwenge


WAHISANI wa Programu ya Maendeleo ya Sekta ya Maji (WSDP), kwa awamu ya pili inayoanza utekelezaji wake mwaka huu, wametoa Sh trilioni tatu ikiwa ni sehemu ya mchango wao katika kuhakikisha kero ya huduma ya maji kwa wananchi inamalizwa.
Waziri wa Maji na Umwagiliaji, Gerson Lwenge alisema hayo jana Dar es Salaam, wakati akifungua mkutano wa 20 wa wadau wa sekta hiyo na kuwataja wahisani hao kuwa ni pamoja na Benki ya Dunia (WB), Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) na Benki ya Ufaransa.

Lwenge alisema, katika kutekeleza programu hiyo awamu ya pili, inayotegemea kuanza mwaka wa fedha 2016/17, wahisani hao wametoa Dola za Marekani bilioni 1.4 (Sh trilioni tatu), na kwamba awamu yote hiyo ya miaka mitano inagharimu kiasi cha trilioni sita.
“Tumeanza vizuri, wahisani wetu wameahidi kutupa kiasi cha takriban Sh trilioni tatu, na bajeti ya wizara kwenye programu hiyo ya maji kwa miaka mitano, tutaiwasilisha bungeni,” Lwenge alisema.

Fedha hizo ni kwa ajili ya kuhakikisha miundombinu ya maji inaboreshwa na maeneo ambayo haipo inajengwa, pia kulinda vyanzo vya maji na kuhakikisha wananchi wengi zaidi wanafikiwa na huduma hiyo muhimu.

Alisema, matarajio ya wizara hiyo ni kumaliza tatizo la maji ifikapo mwaka 2020, jambo alilosema kuwa linawezekana, kwa sababu kwa sasa mamlaka za maji na wizara hiyo zinaendelea na kazi ya kuongeza miundombinu ya maji na kusambaza kwa wananchi.
Alisema, inatarajiwa kuwa hadi ifikapo Machi mwaka huu tatizo la maji kwa wananchi wa mikoa ya Pwani, ikiwemo Dar es Salaam watakuwa wameondokana na tatizo hilo, kwa kuwa uzalishaji maji katika mto Ruvu utakuwa umeongezwa.

Awamu ya kwanza ya Programu ya WSDP, ilianza mwaka 2007 na iliisha Desemba mwaka jana, kwa miradi mbalimbali ya maji katika mikoa tofauti nchini kutekelezwa, hali iliyosaidia kupunguza kero ya huduma hiyo.

Awali, akizungumzia ripoti ya maji kwa mwaka jana, Mkurugenzi wa Programu kutoka Idara ya Uratibu wa wizara hiyo, Dorisia Mulashani alisema, huduma ya maji vijijini na mijini iliendelea kuboreshwa.

0 comments:

Post a Comment