Sunday, January 24, 2016




MAMIA ya wakazi wa Wilaya ya Kinondoni wamejitokeza kupima afya zao ikiwemo ugonjwa wa moyo, katika kampeni iliyoanzishwa na Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, Paul Makonda kwa lengo la kuhamasisha wakazi wa wilaya hiyo kupima afya.

Akizungumza na waandishi wa habari jana jijini Dar es Salaam, Mganga Mkuu wa Wilaya hiyo, Aziz Msuya alisema kuwa wananchi wameitikia mwito huo na wanatarajia kuendelea leo.

Alisema kuwa wingi wa watu waliojitokeza katika kampeni hiyo viwanja vya Leaders, umesababisha kupungukiwa kwa vifaa.

“Mpaka sasa wananchi 2,000 wamepimwa na wengine wanasubiri huduma. Vifaa tulivyokuja navyo vimekuwa pungufu kwa sababu ya wingi wa watu,” alisema Msuya.

Aliongeza kuwa magonjwa yanayopimwa ni kisukari, presha na moyo ambapo baadae wanatakiwa kwenda katika Hospitali ya Mwananyamala au Hospitali ya Taifa ya Muhimbili (MNH).

Pia alitoa wito kwa wakazi hao kutowatoa wagonjwa wao ambao wako hospitali kwani kitendo kinachofanyika katika kampeni hiyo ni kupima na sio kutibu.

0 comments:

Post a Comment