Thursday, January 21, 2016




MWENYEKITI wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) wa Wilaya ya Rorya, Samwel Kiboye amesema hatawavumilia watu ambao wamekuwa wakicheza pool muda wa kazi.

Hayo aliyasema jana kwenye hafla fupi ya sherehe za diwani wa kata ya Koryo, Peter Sarungi kwa tiketi ya CCM ya kuwashukuru wananchi kwa kumchagua kuwa diwani wa kata hiyo.

Katika sherehe hizo zilizofanyika nyumbani kwake katika kijiji cha Koryo, Kiboye alisema uchaguzi umekwisha hivyo hawana budi kuendeleza shughuli za maendeleo wilayani hapo.

Aliwataka madiwani kusimamia vizuri na kuhakikisha wanachukua hatua kwa watu wanaocheza mchezo huo wakati wa kazi.

“Nimemueleza DC (mkuu wa wilaya) ahakikishe vijiwe vinavyofanywa na vijana wanashindwa kufanya kazi vivunjwe haraka kwani kukaa vijiweni ni mwanzo wa uporaji wa vitu ama mali za watu, wamekuwa wakikaa vijiweni bila kufanya kazi lakini ikifika muda wa chakula wanaenda kuwafanyia fujo wazazi wao kwa kuwadai chakula,” alisema.

Aliwataka watendaji vijiji na kata kuhakikisha fedha zilizopelekwa mashuleni zinafanya kazi iliyokusudiwa hususan kuunga juhudi za Rais John Magufuli.

“Fedha zilizoingia katika shule tumesikia walimu hawajatangazia wananchi, hivyo naombeni wananchi msimamie kikamilifu, tunamshukuru Rais kwa uamuzi huu mzuri umesaidia wananchi ambao walishindwa kupeleka watoto wao shuleni kutokana na michango mingi na hali zao kuwa ngumu,” alisema.

Naye Diwani wa Kata ya Milale, Nyawambo Adriano ambaye ni katibu wa madiwani wa wilaya hiyo aliwaomba wananchi kuwapatia ushirikiano, ikiwa ni pamoja na kuchangia nguvu kazi katika shughuli za maendeleo badala ya kuiachia serikali.

Kwa upande wake Diwani wa Kata ya Koryo, Peter Sarungi amewapongeza na kuwashukuru wananchi waliohudhuria kwenye sherehe hizo. Aliwataka wampe ushirikano ili kuendeleza na kumuunga mkono Rais Magufuli katika mikakati ya maendeleo ya nchi.

“Kazi ya serikali ni kumalizia kazi na kutoa mwongozo na taratibu za kazi, hivyo tuondokane na usingizi na dhana za zamani tuliokuwa nao bali tushirikiane ili tujiletee maendeleo na tuweze kubadili mji wetu wa Utegi ili usonge mbele,” alisema diwani Sarungi.

0 comments:

Post a Comment