Saturday, January 2, 2016


 
 
Alianza na Dkt. Abdallah Possi, wakafuata Profesa James Epiphan Mdoe na Mhe. Amon Anastaz Mpanju na kusababisha mshangao wa furaha miongoni mwa wananchi wenye ulemavu kwa kile wanachokitaja kama kukumbukwa katika uongozi wa Serikali ya awamu ya Tano ya Rais Dkt. John Pombe Joseph Magufuli. 
 
Rais alipomteua Dkt. Abdallah Possi kuwa Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu - Sera, kazi, Ajira, Bunge, Vijana na walemavu wengi walifurahi kuona Mtanzania wa kwanza mwenye ualbino anaingia katika Baraza la Mawaziri 
 
Furaha hiyo ilizidi alipowateua Mhe. Amon Anastaz Mpanju mlemavu wa kuona kuwa Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Katiba na Sheria na Profesa James James Epiphan Mdoe kuwa Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Nishati na Madini, ambaye ni mlemavu wa miguu.
 
 Mhe Mpanju, ambaye kitaaluma ni mwanasheria na ambaye pia alikuwa mmoja wa wajumbe wa Bunge la Katiba, alishangaza kila mtu wakati alipokula kiapo mbele ya Rais bila kusoma mahali kama ilivyo desturi. 
 
“Huyu bwana pamoja na ulemavu wake hakika ni mtu wa kazi” alisikika mmoja wa wageni waliohudhuria hafla ya kuapishwa Makatibu Wakuu na Manaibu Katibu wakuu Ikulu siku ya Mwaka mpya. 
 
Akiwa amesindikizwa na mke wake, Mhe. Mpanju alipokea Biblia Takatifu na kuinyanyua juu na kuanza kula kiapo, ingawa mkewe alikuwa ameshika karatasi ya maandiko ya vitone ambayo ilikuwa aitumie. Hata Rais alitabasamu kwa hilo. 
 
Huko mitaani, ambako tukio hilo la kuapishwa Makatibu wakuu lilikuwa likirushwa ‘live’ na vituo kadhaa vya TV na Redio na mitandao, wengi walishikwa na butwaa, huku wakimsifia Rais Magufuli kwa kuwakumbuka watu wenye ulemavu. 
 
Waliendelea kufurahi walipomuona Profesa James James Epiphan Mdoe, ambaye ni msomi aliyebobea katika Kemia,  akisogea mbele kwa mikongojo miwili na kula kiapo cha kuwa Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Nishati na Madini.

0 comments:

Post a Comment